Askofu Thèophile Kaboy Ruboneka wa Jimbo Katoliki la Goma, nchini DRC anasema kwamba,
Padre Jean- Paul Kakule Kyalembera hivi karibuni aliuwawa kikatili Parokiani mwake,
Mweso na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi. Marehemu Padre Kyalembera baada ya
kuhitimisha shughuli na utume wake, jioni wakati wa kufunga mlango wa Kanisa, akagundua
kwamba, kulikuwa na kundi la watu waliokuwa wamejificha Kanisa humo na walipomwona,
wakafyatulia risasi na Padre Kyalembera kupoteza maisha yake Kanisa hapo! Tayari watu
kadhaa wanaotuhumiwa kuhusika na tukio hili wamekwishatiwa mbaroni!
Askofu
Ruboneka anasema, kwa muda mrefu eneo la Goma limekuwa ni uwanja wa fujo na mauaji
ya watu wasiokuwa na hatia kutokana na uwepo wa makundi ya kijambazi pamoja na kuzagaa
kwa silaha: Mapadre na watawa wanaendelea kutishiwa maisha yao na wakati mwingine
wanalazimishwa kutoa fedha, jambo ambalo ni hatari kwa maisha na usalama wa raia.