Kuanzia mwaka 1959, Kanisa linaadhimisha Siku ya Wahispania wanaofanya utume wao Amerika
ya Kusini, sherehe ambayo kwa mwaka 2015 inaadhimishwa tarehe Mosi Machi, yaani Jumapili
ya kwanza ya Mwezi Machi. Wainjilishaji kwa nguvu ya Roho Mtakatifu ndiyo kauli mbiu
inayotolewa na Kardinali Marc Ouellet, Rais wa Tume ya Kipapa kwa ajili ya Amerika
ya Kusini.
Hii ni siku
ambayo Kanisa Katoliki nchini Hispania linawahamasisha waamini na watu wote wenye
mapenzi mema kuonesha mshikamano wa upendo na udugu kwa kuchangia kwa hali na mali
shughuli mbali mbali za kichungaji zinazotekelezwa na Wamissionari kutoka Hispania
huko Amerika ya Kusini.
Takwimu zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya Wamissionari
wapatao 9,000 wanaotekeleza dhamana na utume wao katika nchi za Amerika ya Kusini,
kwa kujikita katika mchakato wa Uinjilishaji mpya. Kardinali Ouellet anasema kwamba,
Siku ile ya Pentekoste, Mitume waliokuwa wamejifungia kwa hofu ya Wayahudi, walipata
nguvu na ari mpya iliyowasukuma kutoka nje ili kumshuhudia Kristo Mfufuka kwa moyo
mkuu bila woga wala makunyanzi, wakathubutu kuwa ni Wamissionari wa kwanza wa Habari
Njema ya Wokovu.
Mchakato huu hauna budi kuendelezwa na Wamissionari wanaoendelea
kujisadaka katika nchi za Amerika ya Kusini kwa kujikita katika Injili ya Furaha na
Ujasiri kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko katika nyaraka zake mbali mbali.
Furaha ni chemchemi inayobubujika kutoka kwa Wainjilishaji, ambao kimsingi wanapaswa
kuwashirikisha wale wanaowainjilisha. Kumbe, Uinjilishaji wa watu hauna budi kujikita
katika furaha, ukarimu na upendo wa dhati, huku Wainjilishaji wenyewe wakionesha ushupavu
wa kutangaza Injili pasi na kukata tamaa wala kuchoka.
Kardinali Ouellet anasema
kwamba, hakuna hata kidogo nguvu ya kimissionari iliyotolewa kwa ajili ya kuwatangazia
Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu kwa upendo na mshikamano itakayoweza kupotea
bure. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, matunda ya Uinjilishaji hayategemei nguvu
na juhudi za kibinadamu. Ni Yesu Kristo anayewapatia nguvu ya kuendeleza mikakati
na shughuli za Uinjilishaji, hadi kuwafikia watu wanaoishi pembezoni mwa maisha, ili
wao pia waweze kuona mwanga wa Injili.
Kanisa linatambua magumu na changamoto
ambazo Wamissionari wanakumbana nazo katika maisha na utume wao; kuna mazingira ambayo
yamekuwa ni kizingiti kikuu cha Uinjilishaji, lakini Wamissionari watambue kwamba,
nguvu, juhudi na maarifa waliyowekeza katika mchakato wa kuwatangazia Watu Injili
ya Furaha hazitaweza kupotea kamwe, kama ilivyo vigumu kupoteza upendo unaobubujika
kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Kardinali Ouellet anawaalika Wamissionari kufanya
hija pamoja na Yesu Kristo kila siku ya maisha yao, huku wakimwachia nafasi Roho Mtakatifu
aweze kuwapatia dira na mwongozo katika utekelezaji wa dhamana hii nyeti. Waendelee
kujikita katika maisha ya sala na tafakari ya Neno la Mungu kwa kutambua kwamba, Yesu
daima yuko pamoja nao kamwe hatawaacha yatima.
Ni jukumu la Wamissionari kuwatangazia
watu Injili ya Kristo hata ikibidi kwenda kinyume cha maelekeo ya kijamii, kwani wao
kimsingi ni sauti ya kinabii. Wamissionari wasikubali kupokwa furaha ya Uinjilishaji
kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko. Wamissionari waanze na kuhitimisha siku
ya maisha na utume wao kwa kukutana na kuzungumza na Yesu Kristo katika Neno na Sakramenti,
ili kuimarisha imani na furaha ya kukutana na Yesu huko Amerika ya Kusini.
Wamissionari
kamwe wasikubali kukatishwa tamaa kutokana na magumu mbali mbali wanayokabiliana nayo,
wawe na ujasiri wa kuanza tena pale wanapodhani kwamba, wameshindwa na kuanguka, huku
wakijitahidi kumwiga Bikira Maria aliyekubali kupokea na kuumwilisha mpango wa Mungu
katika maisha yake. Wamissionari wathubutu kuendelea kuutafakari uso wa Mungu kwa
njia ya huduma makini kwa jirani pamoja na kumwilisha sala katika uhalisia wa maisha
yao ya kila siku.
Kardinali Ouellet anawakumbusha Wamissionari kwamba, wanatumwa
na Mama Kanisa kuwaendelea Watu wa Mataifa, kwani utume wa Kanisa ni kielelezo cha
upendo wa Kristo kwa waja wake. Utume wa Uinjilishaji ni dhamana inayopaswa kutekelezwa
na Watu wa Mungu kwa ajili ya wote pasi ubaguzi wa watu au hali yao ya kijamii. Utambulisho
wa kimissionari ujioneshe katika huduma kwa waamini, kwa kuwatakia mema na furaha
ya kweli.
Kardinali Marc Ouellet anahitimisha ujumbe wake kwa ajili ya maadhimisho
ya Siku ya Wahispania wanaofanya utume wao Amerika ya Kusini kwa kusema kwamba, mlchakato
wa Uinjilishaji Amerika ya Kusini ni changamoto ya kuwaendelea maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa jamii. Wamissionari wajidhaminishe chini ya usimamizi na tunza ya Bikira
Maria, ili kweli juhudi zao za kimissionari ziweze kuwa ni kielelezo cha utii kwa
Mungu Baba Mwenyezi.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.