Maskini na watu wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii wanapaswa kuonjeshwa huruma na
upendo wa Mungu kwa kusoma alama za nyakati ili kumwachia Mwenyezi Mungu nafasi ya
kuwashangaza viongozi wa Kanisa katika maisha na utume wao kama ilivyotokea kwa Nabii
Eliya alivyomshangaza yule Mjane wa Sarepta kwa kumponya mwanaye aliyekuwa amemsababishia
uchungu mkubwa moyoni mwake. Mama Mjane anatambua na kukiri ukuu wa Mungu katika maisha
yake.
Hii ndiyo changamoto ambayo imetolewa na Padre Bruno Secondin wakati
wa tafakari zake kwa Baba Mtakatifu Francisko na wasaidizi wake wa karibu wakati wa
mafungo ya maisha ya kiroho huko Ariccia, nje kidogo ya mji wa Vatican, mafungo ambayo
yalianza Jumapili jioni na kuhitimishwa, Ijumaa asubuhi tarehe 27 Februari 2015, kwa
Ibada ya Misa Takatifu. Hapa Kanisa linawaangalia maskini jinsi wanavyoshiriki kikamilifu
katika mchakato wa Uinjilishaji kwa kujikita katika imani, matumaini na mapendo.
Ni
kundi linaloonesha ukarimu hata katika umaskini wake, kiasi cha kumshangaza Nabii
Eliya ambaye alionekana kuwa na shingo ngumu. Mjane wa Sarepta kwa namna ya pekee,
anawafundisha waamini kwamba, umaskini na fumbo la kifo ni mambo yanayopaswa kushughulikiwa
kikamilifu bila ya kupoteza utu na heshima ya binadamu! Mjane wa Sarepta hatua kwa
hatua anakutana na uso wa Mungu mwenye huruma na mapendo anayekuja kuganga na kuponya
madonda ya machungu katika maisha yake. Hapa haki ya Mungu inajionesha na kumwilishwa
katika uhalisia wa maisha kielelezo makini kwa wafuasi wa Kristo, kwani maskini na
wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii wana upendeleo wa pekee mbele ya Yesu na Kanisa
lake.
Padre Secondin anasema, Nabii Eliya alikuwa ni mtu wa haki na kamwe hakusita
kusema na kusimamia ukweli kiasi hata cha kumkaripia Mfalme Ahazi kwa kumnyang'anya
na kumdhulumu Nabothi shamba ambalo lilikuwa ni urithi kutoka kwa Baba zake. Lakini
ni mara ngapi kilio cha maskini kimeweza kusikiwa na wakuu wa watu? Kilio cha damu
kinaendelea kusikika huko Mashariki ya Kati, Afrika na sehemu mbali mbali za dunia,
lakini watu wamekaa kimya kana kwamba, hakuna kinachotendeka, hiki ni "kilio cha samaki
machozi yamebaki majini"
Padre Secondin anasema, viongozi wa Kanisa kwa kushirikiana
na watu wenye mapenzi mema, hawana budi kuungana ili kulinda, kutetea na kusimamia
haki msingi za maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Ikumbukwe kwamba,
ardhi ni mali ya Mungu kwa ajili ya mafao ya wengi. Toba na wongofu wa ndani vipate
mwanzo wake katika maisha ya viongozi na waamini kwa ujumla kwa kubadili mfumo wa
maisha kwa kuanza kujikita katika ukweli na uwazi; haki na uaminifu kwa kutambua kwamba,
uongozi ni huduma na wala si ndoana ya kujitafutia "ujiko".
Viongozi wa Kanisa
watekeleze dhamana na wajibu wao barabara; kwa kuhamasisha kulinda na kutunza mazingira;
kwa kuwatetea na kuwahifadhi wakulima wadogo wadogo wanaopokonywa ardhi na vyanzo
vya maji kwa ajili ya mafao ya wajanja wachache katika jamii. Viongozi wawe na ari
pamoja na ujasiri wa kupinga nyanyaso, dhuluma na uonevu ndani ya jamii; kwa kushikamana
na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kwa kujikita katika kanuni
msingi za Kiinjili bila woga wala makunyanzi!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.