2015-02-26 12:18:36

Mshikamano wa umoja na udugu katika mapambano dhidi ya umaskini!


Waamini wa dini na madhehebu mbali mbali ya Kikristo wanaweza kushikamana na kusaidiana katika mchakato wa kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo, mshikamano, maendeleo na mafao ya wengi, kwa kutambua kwamba, wote ni wamoja na tofauti zao za kidini na kiimani ni utajiri mkubwa unaopaswa kutumiwa kwa ajili ya wote pasi na misigano wala kinzani za kiimani.

Ni katika mantiki hii, Familia ya Mungu nchini Ethiopia kwa kuzingatia utajiri wa imani za dini na madhehebu mbali mbali yaliyoko nchini humo wanaendelea kushikamana katika mapambano dhidi ya umaskini na misimamo mikali ya kiimani, ambayo kwa miaka mingi imekuwa ni chanzo kikuu cha majanga, sehemu mbali mbali za dunia. Waamini wa Kanisa Katoliki ni sehemu ya idadi ndogo sana ya Familia ya Mungu nchini Ethiopia, lakini wanachangia kwa kiasi kikubwa katika ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ethiopia hususan katika sekta ya elimu, afya na maendeleo jamii yanayozingatia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Hayo yamesemwa hivi karibuni na Kardinali Berhaneyesus Demerew Souraphiel, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Addid Ababa, Ethiopia katika mahojiano maalum na Gazeti la L'Osservatore Romano linalomilikiwa na Vatican. Anasema, Wakristo nchini Ethiopia ni daraja la majadiliano ya kidini na kiekumene; kiasi kwamba, wote wanafanya kazi zao kwa kushirikiana, kuthaminiana na kutegemeana katika medani mbali mbali za maisha.

Kwa miaka mingi Wakristo na Waislam wanaishi kwa amani na utulivu pasi na mikwaruzano wala malumbano yasiyokuwa na tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya wananchi wengi wa Ethiopia. Kumekuwepo na harakati kutoka kwa baadhi ya waamini wenye misimamo mikali ya kiimani waliotaka kuwagawa na kuwagombanisha wananchi wa Ethiopia, lakini watu wengi waliowabeza na wala hawakuwafuata katika nia yao hii mbaya; matokeo yake umoja na mshikamano wa kitaifa unaendelea kudumishwa kama kikolezo cha maendeleo endelevu.

Kanisa Katoliki nchini Ethiopia ni mdau mkubwa wa maendeleo katika sekta ya elimu, afya na ustawi wa jamii anasema Kardinali Souraphiel. Hapa ni mahali pa kukuza na kuendeleza majadiliano ya kiekumene yanayosimikwa katika uhalisia wa maisha; wakati wa furaha na majonzi. Waamini wamefundwa wakaiva katika misingi ya imani na wala hakuna tatizo la kutaka kugombea waamini, kwani mfumo huu wa maisha umepitwa na wakati. Watu wanavuwa na ushuhuda makini wa maisha na wala si kwa upanga wala mambo mengine yanayopita! Imani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayopokelewa kwa moyo wa unyenyekevu na shukrani.

Kardinali Soiraphiel katika maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani anasema kwamba, watawa wanaweza kujipambanua kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; kwa kujikita katika ustawi na maendeleo ya watu kwa njia ya huduma makini inayotolewa na Mashirika mbali mbali ya kitawa na kazi za kitume katika sekta ya elimu, afya na ustawi wa jamii.

Kwa njia hii, watawa wanaweza kuwa kweli ni wadau katika kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili ya Maisha, Furaha na Matumaini kwa kukumbatia tunu msingi za maisha, tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake, hadi mauti ya kawaida yanapomfika kadiri ya mpango wa Mungu. Familia ya Mungu nchini Ethiopia inawaheshimu na kuwathamini sana watawa kutokana mchango wao katika ustawi na maendeleo ya wengi; ni watu wanaojisadaka kuwasaidia wazee, watoto yatima na wale ambao wanatumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.