2015-02-25 15:20:36

Vijana wa kizazi kipya wanataka kuona ushuhuda!


Watawa wanakabiliana na changamoto mbali mbali katika maisha na utume wao katika ulimwengu mamboleo, kiasi kwamba, maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani yanalenga pamoja na mambo mengine kuwasaidia kuangalia historia iliyopita kwa moyo wa shukrani na kuwa na matumaini kwa siku za usoni, kwa kuendelea kuwamasisha vijana wa kizazi kipya, kuona umuhimu wa kujisadaka kwa ajili ya Mungu na jirani zao kwa njia ya maisha ya kitawa!

Hizi ni kati ya changamoto zinazofanyiwa kazi na washiriki wa mkutano wa kimataifa ulioandaliwa na Shirikisho la Mashirika ya Kitawa Kitaifa kutoka Chicago, Marekani, unaofanyika mjini Roma unaofadhiliwa na Mfuko wa Conrad N. Hilton. Padre David Glenday, Katibu mkuu wa Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume nchini Italia anasema, kongamano hili la kimataifa lililofunguliwa Jumatatu, 23 Februari 2015 linawashirikisha wakuu wa mashirika na walezi wa miito kutoka katika mashirika mbali mbali ya kitawa na kazi za kitume.

Lengo ni kujaribu kutafuta majibu muafaka ili kukabiliana na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika maisha ya kitawa bila ya kukata tamaa. Wajumbe wanaendelea kukazia umuhimu wa Kanisa kujikita katika mchakato wa kuimarisha tunu bora za maisha ya ndoa na familia ili kupata Familia imara na thabiti zinazoweza kutoa watoto wenye imani, matumaini na mapendo thabiti, tayari kujisadaka kwa ajili ya Mungu na jirani zao katika maisha ya kitawa au Upadre.

Jambo la kusikitisha ni kuona kwamba, vijana wengi kutokana na changamoto za maisha, wanashindwa kufanya maamuzi magumu katika maisha yao kwa kuacha yote na kumfuasa Kristo katika maisha ya kitawa kama ilivyo vigumu hata katika maisha ya ndoa na familia, Changamoto hizi hazina budi kuangaliwa kwa imani na matumaini pamoja na kuendelea kujielekeza katika ushuhuda makini, malezi ya awali na endelevu kwa ajili ya udumifu.

Padre David Glenday anasema, vijana wa kizazi kipya wanahitaji kuona ushuhuda wenye mvuto na mashiko kutoka kwa watawa; ushuhuda wa furaha na amani ya ndani; ushuhuda unaojionesha kwa watawa kujisadaka kwa ajili ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; ushuhuda unaojikita katika mashauri ya Kiinjili unaomwilishwa katika neema, uhuru na utashi kamili.

Licha ya watawa wengi kukata tamaa na kubwaga manyanga katika maisha haya, lakini bado kuna kundi kubwa la vijana wa kizazi kipya wanataka kujiunga na mashirika ya kitawa na kazi za kitume, jambo la msingi ni kuimarisha utume wa Kanisa miongoni mwa vijana. Kuna cheche za ongezeko la miito mitakatifu nchini Ufaransa na Marekani, huu ni ushuhuda kwamba, kweli Roho Mtakatifu bado anafanya kazi ndani ya Kanisa.

Baba Mtakatifu Francisko ni mfano bora wa kuigwa katika maisha na utume wa Kanisa. Kongamano hili ni matunda ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, changamoto kwa watawa kuishi kikamilifu karama za mashirika yao kwa kuzitolea ushuhuda wenye mvuto na mashiko!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.