2015-02-25 10:32:59

Rushwa na ufisadi visipakwe mafuta kwa mgongo wa chupa!


Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linawataka Wabunge nchini humo kuhakikisha kwamba, wanatunga sheria itakayopambana kwa dhati kabisa na rushwa, ufisadi pamoja na wizi wa mali ya umma, kwani haya ni mambo ambayo kwa sasa ni majanga ya kitaifa na kimataifa. Kupokea na kutoa rushwa ni kishawishi cha watu wengi ndani ya jamii.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada limechapisha Waraka huu wakati ambapo wanasubiri taarifa kutoka Serikali ya Canada kuhusu hali na mwelekeo wa vitendo vya rushwa na ufisadi nchini humo. Hii ni Tume iliyoanzishwa kunako mwaka 2011 ili kuangalia vitendo vya rushwa na ufisadi vinavyoweze kujipenyeza katika masuala ya ujenzi, vyama vya kisiasa na makundi ya uhalifu wa kupanga.

Ni matumaini ya Maaskofu kwamba, taarifa ya tume hii itatoa pia mapendekezo yanayopaswa kufanyiwa kazi ili kung'oa vitendo vya rushwa na ufisadi nchini humo. Rushwa kamwe isipakwe mafuta kwa mgongo wa chupa, bali ishughulikiwe kikamilifu, kwa kuwawajibisha watu katika ukweli na uwazi. Baba Mtakatifu Francisko aliwahi kusema kwamba, watu hawana budi kujenga utamaduni wa kuwajibika ili taratibu rushwa na ufisadi viweze kutokomezwa sehemu mbali mbali za dunia. Juhudi za kwanza ni ujenzi wa dhamiri nyofu pamoja na kuanza mchakato wa kusafisha matendo yanayopelekea watu kutaka kujikita katika rushwa, ufisadi na wizi wa mali ya umma.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kuwa jamii ijenge utamaduni wa haki, amani na usawa kati ya watu wake; wananchi wajifunze kuridhika na mapato halali ya kazi halali wanazofanya. Ili kupambana na rushwa pamoja na ufisadi hatoshi kujikita katika haki na mshikamano wa kidugu, kwa kugawana kile kilichopo, bali kuwa na sheria makini zitakazopambana na rushwa, ili hatimaye iweze kuong'olewa katika maisha ya watu.

Kutokana na kushamiri vitendo vya rushwa na ufisadi, baadhi ya watu wanadhani kwamba, huu ndio mtindo wa maisha ya kisasa, nje ya mambo haya, wewe umepitwa na wakati! Wananchi wajenge ujasiri wa kukataa kutoa au kupokea rushwa, iwe ni ndogo au kubwa kiasi gani! Jamii inawapongeza wale wote ambao hadi wakati huu hawajajihusisha na vitendo vya rushwa na ufisadi, wao ni mfano bora wa kuigwa na mfungamo wa maisha ya kijamii na kwamba, inawezekana mtu kuishi bila ya kupokea au kutoa rushwa wala kuwa fisadi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada limetuma maswali dodoso ili kuangalia hali na mwenendo wa rushwa na ufisadi nchini Canada, ili kweli hatua makini ziweze kuchukuliwa kama sehemu ya mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi, majanga ya kitaifa na kimataifa kwa sasa!







All the contents on this site are copyrighted ©.