2015-02-25 09:59:30

Ondoeni vinyago vyenu, ili muonje upendo na huruma ya Mungu!


Toba na wongofu wa ndani katika Kipindi hiki cha Kwaresima vimsaidie mwamini kuwa mkweli na kujiweka wazi mbele ya Mwenyezi Mungu, tayari kuomba huruma na upendo wake katika hija ya maisha ya kiroho. Ni mwaliko wa kumwilisha utajiri wa tunu msingi za kiroho katika uhalisia wa maisha pasi ya kutafuta visingizio. Kama ilivyokuwa kwa Nabii Eliya aliyelazimika kujionesha mbele ya Mfalme Ahabu ingawa alihofia usalama wa maisha yake, hii ndiyo changamoto hata kwa viongozi wa Kanisa kuchunguza undani wa maisha yao, kusikiliza kwa makini ushauri ambao Mwenyezi Mungu anataka kuwashirikisha na hatimaye, kuufanyia kazi.

Kimsingi hizi ni kati ya changamoto zinazoendelea kutolewa na Padre Bruno Secondin kwa Baba Mtakatifu Francisko na wasaidizi wake wa karibu, wakati huu wanapoendelea na mafungo ya maisha ya kiroho huko Ariccia, nje kidogo ya mji wa Vatican. Wakristo katika ujumla wao wanapaswa kuonesha ujasiri na uthabiti wa imani hasa pale wanapokabiliwa na changamoto za maisha ya imani. Kanisa lioneshe ari na ujasiri wa kuwatangazia Watu wa Mungu kweli za maisha pasi na woga wala makunyanzi wala kutafuta kumfurahisha mtu, kwani ukweli unauma na kuponya!

Viongozi wa Kanisa wasimame kidete kulinda na kutetea ukweli, hata kama itawabidi kujisadaka maisha yao, kwani huu ndio utume wa kinabii ambao Mama Kanisa anaalikwa kuutolea ushuhuda makini, katika hali ya unyenyekevu, daima kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu. Ni wajibu wa Kanisa kuwasaidia, kuwatetea na kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, Kanisa litambua kwamba, rasilimali fedha, vitu na watu ni kwa ajili ya kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji na wala si mali ya mtu binafsi.

Viongozi wa Kanisa wawashirikishe waamini wao katika maisha na utume wa Kanisa kama alivyofanya nabii Eliya wakati alipokuwa anakabiliwa na majaribu katika maisha. Pengine umekuwa ni utamaduni kwa baadhi ya viongozi wa Kanisa kufanya maamuzi makubwa ya maisha na utume wa Kanisa kwa kuwahusisha watu wachache, lakini, changamoto za Uinjilishaji mpya zinawataka viongozi wa Kanisa kuthubutu kuishirikisha yote ya Mungu, pengine kwa njia ya uwakilishi mpana zaidi.

Hapa wazo linaloibuliwa ni kuanza kujenga utamaduni wa kufanya, kupembua, kupanga na kutekeleza maamuzi kwa njia ya kuwashirikisha watu. Kanisa litambue mapungufu yake ya kibinadamu na kuwa na ujasiri wa kuyakiri pasi na woga; liangalie pale ambapo limeshindwa kutenda haki, ili kuomba huruma na msamaha, tayari kuanza mchakato wa uponyaji wa ndani.

Historia ya Kanisa anasema Padre Bruno Secondin inaonesha pia kwamba wakati fulani, Kanisa liliwatesa na kuwanyanyasa watu, pengine madhulumu haya leo hii yanaweza kuwa katika mtindo tofauti wa maisha kwa maneno au kwa kutumia mitandao ya kijamii. Hapa kunahitajika toba na wongofu wa ndani, ili kuona ukweli baada ya kuchunguza dhamiri mbele ya Mwenyezi Mungu, katika uhuru kamili, ili kutoa nafasi kwa Mungu aweze kuwafunda na kuwaponya kutoka katika undani wa maisha yao.

Padre Secondin anasema, maneno matupu hayawezi kamwe kujenga na kuimarisha imani, kwani mwelekeo kama huu mara nyingi ndani mwake kuwa mambo ambayo yamefichika yaani: kiburi, tamaa ya madaraka, mafanikio katika elimu na huduma; lakini hata katika miungu hii midogo, bado huruma na upendo wa Mungu aliye hai ni mkuu na unaweza kuunguza na kuwaponya kutoka katika undani wao, kama ilivyokuwa kwa Nabii Eliya, akafaulu kujenga utambulisho wa Waisraeli kwa njia ya Makabila kumi na mawili, kwani Mwenyezi Mungu ni mwaminifu kwa ahadi zake na yupo daima kwa wale wote wanaomkimbilia.

Padre Bruno Secondin anawaalika viongozi wa Kanisa kuamsha tena dhamiri nyofu miongoni mwa Familia ya Mungu, kwa kuwa na mikakati na dira makini katika shughuli za kichungaji, maisha na utume wa Kanisa; kwa kumwachia Mungu nafasi katika maisha na mipango yao, daima wakiendelea kumshirikisha kwa njia ya sala.

Nabii Eliya kama anavyosimuliwa na Mtakatifu Efrehemu ni kielelezo cha Yesu katika Agano Jipya, hali inayoonesha: Fumbo la Umwilisho, Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Yesu hadi kupaa kwake mbinguni anakoishi mkono wa kuume wa Baba yake wa Mbinguni. Yesu ni kielelezo na mfano wa maisha yanayojikita katika: ufukara, utii na useja; mwaliko kwa Familia ya Mungu kuchuchumilia amani na utakatifu wa maisha, huku wakiendelea kuwa waaminifu mbele ya Mwenyezi Mungu. Waamini katika maisha yao, wajibidishe kuitafuta mbingu, ili waweze kupata maisha ya uzima wa milele.

Padre Bruno Secondin anasema unga na mafuta aliyotumia Nabii Eliya kufanya muujiza ni kielelezo cha huruma na upendo wa Mungu kwa waja wake; mwaliko kwa viongozi wa Kanisa kuwa makini kwani wanaweza kukumbana na Mbwa mwitu katika maisha na utume wao; wawe wapole na wanyenyekevu katika kuchunga Kondoo wa Kristo. Wawasaidie waamini wao kuwaosha kwa maji ya Ubatizo na kuwapaka mafuta ya huruma ya Mungu kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho. Kwa ufupi, haya ndiyo mawazo makuu ambayo yanaendelea kutawala katika mafungo yanayotolewa na Padre Bruno Secondin kwa Baba Mtakatifu Francisko pamoja na wasaidizi wake wa karibu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP. S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.