2015-02-25 10:23:13

Mapambano dhidi ya biashara haramu ya dawa za kulevya!


Padre Federico Lombardi anasema kwamba, Baba Mtakatifu Francisko anaunga mkono mapambano dhidi ya biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya yanayofanywa na watu mbali mbali na kwamba, matumizi ya maneno "evitar la mexicanizacion" katika ujumbe aliomwandikia rafiki yake kutoka Argentina hauna uhusiano wowote na wananchi wa Mexico, bali ni msemo uliokuwa umetumiwa kwenye e mail yake binafsi kutoka kwa rafiki yake. Ufafanuzi huu umetolewa kwenye Ubalozi wa Mexico mjini Vatican.

Baba Mtakatifu anawapenda, anawaheshimu na kuwathamini wananchi wa Mexico na kwamba, anapenda kuwaalika wananchi na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete kupinga biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya kwani yana madhara makubwa kwa jamii. Mexico na Amerika ya Kusini katika ujumla wake ni eneo ambalo limeathirika sana kwa biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya.

Kumbe, mapambano dhidi ya biashara hii hayana budi kupewa kipaumbele cha pekee na Serikali pamoja na wadau mbali mbali, ili kupambana na vita pamoja na ukosefu wa amani, jambo linachochewa kwa kiasi kikubwa na biashara haramu ya dawa za kulevya.

Baba Mtakatifu Francisko kwa nyakati na mara kwa mara alipokutana na kuzungumza na Maaskofu amekazia umuhimu wa Jumuiya ya Kimataifa kuwa na mikakati na sera makini za kupambana na biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya kwa kushirikiana kwa vitendo.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican







All the contents on this site are copyrighted ©.