Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameondoka
tarehe 25 Februari, 2015 kuelekea Lusaka Zambia kwa ajili ya ziara ya kikazi ya siku
mbili kufuatia mwaliko kutoka kwa Rais Edgar Chagwa Lungu wa Zambia. Viongozi hao
wanatarajia kufanya mazungumzo kuhusu ushirikiano wa nchi mbili hizi ikiwemo suala
la reli ya Tanzania-Zambia Railway Authority (TAZARA), inayounganisha Tanzania na
Zambia.
Hivi karibuni Reli ya TAZARA imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali
ambazo zinahitajika kujadiliwa kwa kina na viongozi wakuu ili kuimarisha zaidi reli
hiyo ambayo ni kiungo kikubwa baina ya nchi hizi katika masuala ya uchumi na alama
ya ushirikiano.
TAZARA ilizinduliwa rasmi Oktoba 1975 kwa ufadhili wa China.
Reli hiyo ina upana wa milimita 1,067 na urefu wa Kilometa 1, 860 kuanzia Dar es Salaam,
Tanzania na kuishia katika mji wa New Kapiri Mposhi nchini Zambia. Reli hiyo ina uwezo
wa kusafirisha mizigo ya tani milioni 5 na watu milioni 3 kwa mwaka. Rais Kikwete
na ujumbe wake wanatarajiwa kurejea nchini kesho tarehe 26 Februari, 2015.