Katika maadhimisho ya Mwaka wa Maskini nchini Ufilippini waamini na watu wote wenye
mapenzi mema wanaalikwa kujenga mshikamano wa upendo na udugu, ili kuong'a tofauti
za matabaka ambazo zimekuwa ni chanzo za kinzani za kijamii na ukosefu wa amani na
maridhiano nchini humo. Jamii isiwaguezie maskini kisogo, bali ihakikishe kwamba,
maskini wanasaidiwa kupata mahitaji yao msingi katika maisha.
Ni changamoto
inayotolewa na Kardinali Louis Tagle, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Manila, Ufilippini
wakati huu wa maadhimisho ya Kipindi cha Kwaresima. Hapa kuna haja kwa Familia ya
Mungu nchini Ufilippini kujifunga kibwebwe ili kupambana na ubinafsi pamoja na uchoyo
mambo ambayo yanawafanya watu kugubikwa na utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko
ya jirani zao.
Watu wajitahidi kupambana kufa na kupona na ukosefu wa haki
msingi za kijamii, rushwa na ufisadi; baa la njaa na utapiamlo wa kutisha miongoni
mwa watoto wenye umri chini ya miaka sita, ambao wengi wao wanafariki dunia kwa kukosa
chakula bora. Haya ni mambo ambayo yako ndani ya jamii, kumbe, kipindi cha Kwaresima
kiwasaidie watu kufanya toba na wongofu wa ndani, tayari kuwaonjesha jirani zao upendo
na huruma ya Mungu.
Hiki ni kipindi kinachowahamasisha waamini kuyapyaisha
maisha yao ya kiroho kwa njia ya sala na tafakari ya Neno la Mungu inayomilishwa katika
matendo ya huruma. Hapa waamini washiriki kikamilifu katika sera na mikakati ya Jimbo
katika mapambano dhidi ya baa la njaa na utapiamlo. Sala wakati wa Kwaresima inakwenda
sanjari na umwilishaji wa mshikamano wa upendo na udugu, ili kukuza na kudumisha amani
na maridhiano kati ya watu.
Wananchi wanahamasishwa kuwasaidia na kuwahudumia
maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii sanjari na utunzaji bora wa mazingira
kwani athari za mabadiliko ya tabianchi bado zinaendelea kuwatumbukiza wananchi wengi
katika lindi la umaskini wa hali na kipato pamoja na magonjwa ya mlipuko. Waamini
na watu wote wenye mapenzi mema, wajitahidi kutomezwa na utamaduni wa utandawazi usiojali
wala kuguswa na mahangaiko ya watu kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.