2015-02-24 09:45:33

Acheni woga usiokuwa na msingi!


Mashambulizi ya kigaidi yanayoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali za dunia, yanawajengea watu hofu ya usalama wa maisha yao, kiasi hata cha kutothubutu kupanga safari za hija kama ilivyokuwa hapo awali wakati wa Kipindi cha Pasaka. Lakini, watu hawana budi kuvunjilia mbali woga usiokuwa na msingi, lakini pia vyombo vya ulinzi na usalama kitaifa na kimataifa havina budi kutekeleza dhamana na wajibu wake barabara, vinginevyo, watu wachache wanaopandikiza mbegu ya chuki na hofu miongoni mwa jamii wanaweza kufanikisha azma yao kama jamii haitakuwa makini kupambana nao kikamilifu.

Kwa sasa kuna picha za propaganda zinazooneshwa kwenye mitandao ya kijamii kuonesha ukatili mkubwa unaofanywa huko Mashariki ya kati, kiasi cha watu kubaki wakiwa wameshikwa bumbuwazi kutokana na ukatili huu usiokuwa na chembe ya huruma! Viongozi wa Kanisa katika Nchi Takatifu wanawaalika mahujaji na watu wenye mapenzi mema kutositisha kufanya hija za maisha ya kiroho katika maeneo matakatifu, kwani hiki ni kielelezo cha ushuhuda wa udugu na mshikamano wa kweli wakati wa raha na machungu.

Mahujaji katika maeneo matakatifu wamekuwa ni vyombo vya matumaini kwa Wakristo huko Mashariki ya Kati wanaoendelea kuteswa, kudhulumiwa na kunyanyaswa kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Mauaji ya kikatili na ukosefu wa ulinzi na usalama ni kati ya mambo ambayo yanaendelea kuwatia shaka watu wengi kupanga safari ili kutembelea maeneo matakatifu kwa kuhofia hatima ya maisha yao.

Lakini viongozi wa Kanisa wanasema kwamba, Yerusalemu na Bethlehemu ni maeneo ambayo yako salama hadi sasa, kumbe, mahujaji hawana haja ya kuwa na wasi wasi na kwamba, kuna mahujaji bado wanaendelea kufanya hija zao kwenye Nchi Takatifu. Viongozi wa Kanisa wanawaalika kutembelea maeneo matakatifu kwani ni salama.

Ili kusaidia mahujaji wasiokuwa na uwezo mkubwa kufanya hija katika maeneo matakatifu, hususan vijana, Kanisa mjini Yerusalemu limeamua kuanzisha kituo cha hija, ambacho hapo tarehe 17 Februari 2015, Patriaki Fouad Twal wa Yerusalem alibariki jiwe lake la msingi, ili ujenzi uanze mara moja na kwamba, kitaitwa "Kituo cha Hija cha Papa Francisko" na kinajengwa kwenye mji wa Beit Jala, karibu na mji wa Bethlehemu. Kazi ya ujenzi inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka 2015, ili vijana waweze kuanza kukitumia kituo hiki hapo mwakani.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.









All the contents on this site are copyrighted ©.