Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema anakubaliana na ombi la wakazi wa Nyanzwa
na Igunda wilayani Kilolo, mkoani Iringa kuhusu ujenzi wa bwawa la kuhifadhia maji
yatakayovunwa msimu wa mvua ili yasaidie kuongeza eneo la mradi wa umwagiliaji. Ametoa
kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati akiwahutubia wakazi wa vijiji vya Nyanzwa na Igunda,
mara baada ya kukagua mradi wa umwagiliaji wa Nyanzwa ambao ni maarufu kwa kilimo
cha vitunguu.
“Huu mradi ni wa siku nyingi. Nimewauliza wataalamu niliokwenda
nao wakasema ujenzi wa bwawa ndiyo suluhisho pekee la kuokoa mradi huu na kwamba ni
jambo linalowezekana kama fedha zipo.” Aliutaka uongozi wa mkoa uandae mpango kazi
na wauweke kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha ili mradi huo uweze kuombewa fedha
kwenye bajeti kuu ya Serikali. ia aliwataka wakazi wa eneo hilo wakitunze chanzo cha
maji kwa kuweka mipaka ili watu wasikivamie na hatimaye kukiharibu.
“Tengeni
eneo kwa kuweka mipaka. Mkurugenzi simamia uwekaji wa mipaka kwenye chanzo hiki ili
tukilinde kwani uharibifu wa mazingira utakiharibu kabisa,” alisisitiza. Akiwa katika
ukaguzi wa eneo la mradi, Waziri Mkuu alikutana na mkulima mmoja wa vitunguu Bw. Furaha
Ngalali (32) ambaye alimweleza kwamba mwaka jana alifanikiwa kulima ekari tatu za
vitunguu ambazo zilimpatia kiasi cha milioni 6/- huku kila gunia akiwa ameliuza kwa
sh. 70,000/-.
“Gharama kwa kila ekari ni karibu sh. 600,000/- kwa hiyo kwa
ekari tatu ni sh. milioni 1.8/-. Tukivuna vitunguu tunaandaa bustani ya mbegu na pia
humu tunapanda maharage,” alisema Bw. Ngalali alpoulizwa Waziri Mkuu analima eneo
hilo mara ngapi kwa mwaka. Alipoulizwa soko la vitunguu wanapata wapi, Bw. Ngalali
alisema wanunuzi huwa wanavifuata huko huko Nyanzwa na kwamba wengi wao hutoka Dar
es Salaam, Mbeya na Songea. Kijiji cha Nyanzwa kipo umbali wa kilometa 36 kutoka Ruaha
Mbuyuni ilipo barabara kuu ya kuelekea Dar es Salaam na Mbeya.
Katika hatua
nyingine, Waziri Mkuu amewataka wakazi wa vijiji vya Nyanzwa na Igunda wajikite kwenye
ufugaji wa nyuki kwani hauna gharama kubwa na unawawezesha wananchi kuinua kipato
chao kwa haraka. “Wakati mkisubiri ujenzi wa bwawa ili muongeze uzalishaji wa mbogamboga
ni vema mkaangalia suala la ufugaji nyuki… licha ya kutumika kama sehemu ya kujiingizia
kipato, pia ufugaji nyuki ni njia mojawapo ya utunzaji wa misitu,” alisema.
“Hapa
mlipo kuna msitu mkubwa wenye migunga na mibuyu mingi tu. Yote hii imechanua maua
mengi mno. Lazima tutumie uwepo wa misitu hii kama fursa ya kipekee ya kujiingizia
kipato kwa kuweka mizinga ya nyuki. Unaweza usipate mahindi au vitunguu lakini asali
ikawasaidia kuwapa kipato. Hivi sasa lita moja ya asali imefikia sh. 15,000/- hadi
sh. 20,000/- na tena mtapata nta ambayo pia ina bei nzuri tu,” alisema.
Alisema
kwa sasa asali inauzwa kwa bei ghali kwenye nchi mbalimbali baada ya kuongezeka kwa
mahitaji yake na hasa ikizingatiwa kwamba inatumika kama dawa ya kutibu magonjwa mbalimbali
na pia kwenye baadhi ya vipodozi.
Mapema, akisoma taarifa mbele ya Waziri Mkuu,
Mtendaji wa Kijiji cha Nyanzwa, Bw. Hekima Masanula alisema skimu ya umwagiliaji ya
Nyanzwa ilijengwa mwaka 1960 wakati huo kwa kutumia banio la miti na magunia ya mchanga.
Ilikuja kuboreshwa miaka ya 90 kwa ufadhili kutoka Jumuiya ya Ulaya na Serikali ya
Sweden. “Hata hivyo, skimu hii ambayo inahudumia wakulima 3,469 wakiwemo wanaume 1,662
na wanawake 1,807; inakabiliwa na uhaba wa maji kwani ni hekta 256 tu ambazo zinamwagiliwa
kwa sasa wakati eneo lote la mradi ni hekta 940,” alisema Bw. Masanula.
Alisisitiza
ombi la kujengewa bwawa kama njia pekee ya kuwakwamua wakazi hao kutokanana shida
ya maji inayowapata hasa wakati wa kiangazi.
Wakati huo huo Waziri Mkuu Mizengo
Pinda ameutaka uongozi wa mkoa wa Iringa uangalie uwezekano wa kuanzisha Halmashauri
mpya katika wilaya ya Kilolo kata ya Mahenge na tarafa ya Mahenge kwa sababu ya hali
ya kijiografia ya eneo hilo. “Makao makuu ya wilaya hii yako Kilolo kule milimani.
Ukitaka kuja huku ni lazima upite kwanza mjini ndipo ufike huku. Hapana! Hatuwezi
kuwasaidia wananchi hawa kujiletea maendeleo kwa staili hii,” alisema Waziri Mkuu.
Alikuwa
akihutubia wakazi wa vijiji vya Nyanzwa na Igunda wilayani Kilolo, Jumamosi, Februari
21, 2015) mara baada ya kukagua mradi wa umwagiliaji wa Nyanzwa ambao ni maarufu kwa
kilimo cha vitunguu. Vijiji hivyo viko umbali wa km. 120 kutoka Ipogoro ilipo njia
panda ya kwenda Iringa mjini na km. 155 kutoka Kilolo mjini yalipo makao makuu ya
wilaya hiyo.
Waziri Mkuu alisema kata za tarafa hiyo ni kubwa mno kwa mtendaji
kuweza kusukuma maendeleo ya wananchi. “Kata hii imeanzia Kitonga hadi huku Nyanzwa.
Hivi ni mtendaji gani anayeweza kuja kuhimiza shughuli za maendeleo akitokea huko?”
alihoji Waziri Mkuu huku akishangiliwa. Alisema mbali na idadi ya watu, suala la kijiografia
huwa linaangaliwa wakati wa kuanzisha maeneo ya utawala. “Hili eneo ni zuri, fursa
zipo lakini linakosa usimamizi ndiyo maana hata wilaya hii inaongoza kwa umaskini
kuliko wilaya nyingine za mkoa huu. Acheni wilaya ibaki moja, mbunge abaki mmoja lakini
Halmashauri ziwe mbili ili muweze kusukuma maendeleo ya eneo hili kwa sababu mtakuwa
na madiwani wenu na bajeti yenu,” alisema.
Mapema, akisoma taarifa mbele ya
Waziri Mkuu, Mtendaji wa Kijiji cha Nyanzwa, Bw. Hekima Masanula Katemo alisema skimu
ya umwagiliaji ya Nyanzwa ilijengwa mwaka 1960 wakati huo kwa kutumia banio la miti
na magunia ya mchanga. Ilikuja kuboreshwa miaka ya 90 kwa ufadhili kutoka Jumuiya
ya Ulaya na Serikali ya Sweden.
“Hata hivyo, skimu hii ambayo inahudumia wakulima
3,469 wakiwemo wanaume 1,662 na wanawake 1,807; inakabiliwa na uhaba wa maji kwani
ni hekta 256 tu ambazo zinamwagiliwa kwa sasa wakati eneo lote la mradi ni hekta 940,”alisema
Bw. Masanula. Waziri Mkuu anaendelea na ziara yake mkoani Iringa kwa kutembelea
Manispaa ya Iringa ambako atakagua ujenzi wa maabara kwenye shule ya sekondari Kihesa,
kuzindua kituo cha polisi cha Semtema, na kukagua huduma za afya kwenye hospitali
ya manispaa ya iringa. Pia atakagua mradi wa machinjio ya kisasa ya Ngelewela kabla
ya kuhutubia mkutano wa hadhara kwenye viwanja wa shule ya msingi Ipogolo.