2015-02-23 09:20:04

Wako Jangwani wanapambana kiume!


Baba Mtakatifu Francisko pamoja na wasaidizi wake wa karibu, Jumapili jioni tarehe 22 Februari 2015 wameanza mafungo ya maisha ya kiroho yanayoongozwa na Padre Bruno Secondin, Jaalim mstaafu wa tasaufi mamboleo na maisha ya kiroho kutoka Chuo kikuu cha Kipapa cha Gregorian, kilichoko mjini Roma. Mafungo haya yatakamilika hapo Ijumaa, tarehe 27 Februari 2015.

Mafungo haya anasema Padre Bruno kutoka Shirika la Wakarmeli kwamba, yanaongozwa na maneno ya Nabii Elia, moja ya Manabii wakuu wa Agano la Kale, aliyeonesha uaminifu mkuu mbele ya Mwenyezi Mungu licha ya madhulumu na nyanyaso alizokumbana nazo katika hija ya maisha yake hapa duniani. Akakimbilia Jangwani, ili afunikwe na kifo, lakini huko akashibishwa na mkate wa ajabu na kuzima kiu yake kwa maji yaliyotoka mwambani, kiasi hata cha kumwezesha kustahimili adha ya jangwani kwa muda wa siku arobaini, hadi siku ile alipofanikiwa kuupanda Mlima wa Oreb na hatimaye, akakutana na Mwenyezi Mungu, katika hali yake ya unyonge na udhaifu.

Padre Bruno anasema mafungo haya ni changamoto ya kutaka kurejea tena katika mizizi ya maisha ya kiroho, ili kuwa na ujasiri wa kukataa maisha ya undumilakuwili pamoja na kukumbatia miungu wadogo wadogo badala yake kuwa na ibada ya kweli kwa kumwachia nafasi Mwenyezi Mungu ili aweze kuwashangaza katika hali ya ukimya na kwamba, maskini wanayo nafasi ya pekee katika kuwainjilisha Watu wa Mataifa. Kutokana na mantiki hii, Wakristo hawana budi kuwa kweli ni mashuhuda wa haki na mshikamano; unabii na udugu.

Padre Bruno anasema, tafakari zake zitaongozwa na maisha ya sala, ili kuwasaidia wahusika kumwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao. Neno la Mungu ni chakula cha maisha ya kiroho, ambacho utamu wake ni endelevu. Kipindi hiki cha Mafungo ya kiroho kwa Baba Mtakatifu Francisko na wasaidizi wake wa karibu, hatafanyaKatekesi yake siku ya jumatano na mazungumzo binafsi kwa sasa yamesitishwa hadi pale watakaporudi kutoka Jangwani!







All the contents on this site are copyrighted ©.