2015-02-21 16:24:25

Wahudumieni wagonjwa kwa upendo na huruma!


Askofu mkuu Robert Ndlovu wa Jimbo kuu la Harare, Zimbabwe katika barua yake ya kichungaji wakati huu wa Kwaresima anawataka waamini kuwakumbuka, kuwasaidia na kuwahudumia wagonjwa kwa moyo wa upendo na ukarimu, kwa kutambua kwamba, Kwaresima ni kipindi cha toba na wongofu wa ndani, kinachojikita katika matendo ya huruma. Ni wakati muafaka wa kuikimbia dhambi na nafasi zake, ili kushikamana na kuandamana na Mwenyezi Mungu, mwingi wa huruma na mapendo.

Kwaresima, iwasaidie waamini kuonesha mshikamano wa pekee na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kutokana na sababu mbali mbali za maisha; hawa ni watu ambao hata wakati mwingine, wanapewa kisogo na Kanisa.

Askofu mkuu Ndlovu anasema, Kanisa halina mbadala katika kutoa huduma hasa kwa wagonjwa na maskini. Hawa ni watu ambao wanateseka kiroho na kimwili, kumbe kuna haja kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwasaidia na kuwahudumia kwa upendo na huruma, kwani hii ni sehemu muhimu sana ya shughuli na mikakati ya kichungaji inayotekelezwa na Mama Kanisa ambalo bado linapenda kuwekeza katika sekta ya elimu na majiundo makini ya binadamu: kiroho na kimwili.

Kanisa limeendelea kuwa mstari wa mbele kwa kuwasaidia waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi; watoto yatima na wale wote wanaoishi katika mazingira hatarishi na kwamba, Kanisa pia linachangia katika tafiti mbali mbali zinazolenga kuleta mabadiliko katika maisha ya watu. Huduma ya afya inayotolewa na Mama Kanisa haina budi kumsaidia mtu mzima: kiroho na kimwili, ili kuwaonjesha huruma na upendo wa Mungu kama anavyosema Kristo mwenyewe "nilikuwa mgonjwa, ukaja kunitazama na kuhudimia". Kile ambacho waamini wanajinyima kama sehemu ya sadaka na mfungo wao wa Kwaresima kiwasaidie wagonjwa kupata tiba muafaka mahali walipo.

Baba Mtakatifu Francisko katika Ujumbe wake wa Kwaresima anawahamasisha waamini kujenga na kuimarisha mshikamano wa upendo na udugu, kwa njia ya huduma makini kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Ni mwaliko wa kuachana na utandawazi usioguswa wala kujali mateso na mahangaiko ya wagonjwa. Sadaka ya Kwaresima kwa mwaka huu Jimbo kuu la Harare, Zimbabwe itatumika kwa ajili ya maboresho ya huduma ya afya Jimboni humo. Askofu mkuu Robert Ndlovu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusali na kuwaombea wagonjwa bila kusahau kuwahudumia kwa moyo wa huruma na upendo!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.









All the contents on this site are copyrighted ©.