2015-02-21 16:35:18

Kongamano la Watawa Duniani!


Mama Kanisa anaendelea kuadhimisha Mwaka wa Watawa Duniani kwa shughuli mbali mbali ili kuonesha mchango wa watawa katika maisha na utume wa Kanisa, hasa wakati huu, Kanisa linapoadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha Waraka wa juu ya Upendo mkamilifu, Perfectae caritatae.

Ni kipindi cha kuchambua na kujiwekea sera na mikakati ya kichungaji kwa ajili ya kuhamasisha na kuendeleza miito mitakatifu ndani ya Kanisa kutokana na ukweli kwamba, kuna Mashirika ya kitawa na kazi za kitume ambayo yako hoi kutokana na uhaba wa miito. Kwa kutambua changamoto hizi, Shirikisho la Watawa Kitaifa kutoka Chicago, nchini Marekani ambalo kwa zaidi ya miaka 27 limejielekeza katika kuhamasisha, kukuza na kuhudumia miito, limeandaa kongamano la kimataifa litakaloanza kutimua vumbi mjini Roma kuanzia tarehe 23 hadi tarehe 27 Februari, 2015 kama sehemu ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani.

Lengo la Kongamano hili ni kutaka kubadilishana: uzoefu na habari na kuabinisha mbinu na mikakati inayoweza kutumiwa na Mashirika mbali mbali ya kitawa na kazi za kitume katika kuhamasisha miito ya kitawa. Kongamaono hili litawashirikisha walezi na wakuu wa Mashirika ya kitawa na kazi za kitume kutoka sehemu mbali mbali za dunia pamoja na baadhi ya maafisa kutoka Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.