2015-02-21 16:31:53

Kipaumbele ni baa la njaa na umaskini duniani!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 21 Februari 2015 amekutana na kuzungumza na Chansella Angela Merkel na ujumbe wake kutoka Ujerumani ambaye baadaye alifanya mazungumzo pia na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Paul Richard Gallagher, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican

Baba Mtakatifu pamoja na mgeni wake wamezungumzia masuala ya kimataifa na kikanda kwa kujielekeza zaidi katika mkutano wa wakuu wa Nchi Saba tajiri duniani, maarufu kama G7 utakaofanyika nchini Ujerumani; mapambano dhidi ya baa la njaa na umaskini; biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo pamoja na haki za wanawake duniani.

Viongozi hawa wawili wameangalia kwa pamoja changamoto zinazoendelea kuikabili Jumuiya ya Kimataifa sanjari na utunzaji bora wa mazingira, haki msingi za binadamu na uhuru wa kuabudu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kwa kukazia umuhimu wa kudumisha tunu msingi za maisha ya kiroho kama nguzo ya maridhiano na amani kati ya watu.

Baadaye Baba Mtakatifu na mgeni wake wamejikita zaidi kuhusu hali ya Bara la Ulaya pamoja na kuhakikisha kwamba, Jumuiya ya Ulaya inajibidisha zaidi ili kupata suluhu ya mgogoro wa vita nchini Ukraine.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.