2015-02-20 09:40:01

Wasaidieni waamini kukua kiroho!


Mazungumzo kati ya Baba Mtakatifu Francisko na Wakleri wa Jimbo kuu la Roma, Siku ya Alhamisi, tarehe 19 Februari 2015 yamefanyika katika hali ya faragha, ili kumpatia Baba Mtakatifu nafasi ya kuweza kuwafunda barabara Wakleri wenzake, ili waweze kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa kwa moyo wa ibada, ari na unyenyekevu mkuu, wakitambua kwamba, wao wanayo dhamana ya kuwatangazia na kuwaadhimishia Watu wa Mungu, Mafumbo ya Kanisa.

Mapadre wanapaswa kuihudumia Familia ya Mungu kwa ukarimu na unyenyekevu mkuu unaoshuhudiwa katika uhalisia wa maisha ya Wakleri wenyewe. Wakleri wa Roma wanamshukuru Baba Mtakatifu kwa kuwapatia Waraka wake wa kichungaji wa Injili ya Furaha ambao kwa sasa ni Mwongozo na dira ya mikakati na shughuli za kichungaji kwa Makanisa mahalia.

Ni Waraka unaohamasisha waamini kujisadaka kwa ajili ya kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili ya Furaha kwa njia ya ushuhuda wa maisha yanayomwilishwa katika imani. Haya yamesemwa na Kardinali Agostino Vallini Makamu wa Askofu Jimbo kuu la Roma wakati akimkaribisha Baba Mtakatifu Francisko kuzungumza na Wakleri wa Jimbo kuu la Roma, ili aweze kuwapatia changamoto zitakazowasaidia kuboresha mahubiri wakati wa maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu.

Kardinali Vallini anasema, mahubiri yasiyokuwa na mvuto wala mashiko kwa watu katika ukuaji wao wa maisha ya kiroho, yanachosha. Wakleri ambao wanadhama ya kuhubiri Neno la Mungu walitaka kupata ushauri kutoka kwa Baba Mtakatifu, ili uweze kuwasaidia katika mchakato wa maboresho ya mahubiri yao, ili kuzima kiu na udadisi wa waamini wakati wa maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu. Huu ni mchakato wa shughuli za kichungaji unaolenga kumsaidia Padre kuwa karibu zaidi na Familia ya Mungu kwa njia ya mahubiri yanayomwilishwa katika maisha na vipaumbele vyake.

Maadhimisho ya Mafumbo ya Kanisa yapate chimbuko lake katika uhalisia wa maisha yanayoshuhudia imani tendaji na ari ya kutaka kuwahudumia Watu wa Mungu kwa kuwa na busara, ili kuwasaidia waamini katika hija ya maisha yao ya kiroho.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.