2015-02-20 09:30:05

Usione vinaelea...!


Askofu mkuu mstaafu James Odongo, hapo tarehe 21 Februari 2015 ataadhimisha kilele cha Jubilee ya Miaka 50 tangu alipowekwa wakfu kuwa Askofu, kwenye Kanisa kuu la Mashahidi wa Uganda, Jimbo Katoliki la Tororo, Uganda na muda mfupi baadaye, akashiriki katika maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican uliokuwa unaendelea mjini Vatican, matendo makuu ya Mungu.
Padre Joseph Healey, Mmissionari wa Maryknow ambaye kwa miaka mingi ameishi na kufahnya utume wake katika Nchi za AMECEA, anasema, hadi wakati huu, kuna Maaskofu watatu kutoka katika Nchi za AMECEA walioshiriki katika maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, hawa ni pamoja na: Askofu mkuu mstaafu James Odongo, Askofu mstaafu Colin Davies wa Jimbo Katoliki Ngong, Kenya pamoja na Askofu mstaafu Gervas Placidus Nkalanga wa Jimbo Katoliki Bukoba ambaye kwa sasa anaendelea na maisha ya sala na tafakari katika Monasteri ya Hanga, Jimbo kuu la Songea.
Itakumbukwa kwamba, Kikao cha nne na cha mwisho cha maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, kilijadili na kuchapisha nyaraka kumi na moja, kati ya nyaraka kumi na sita, zilizotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican: Gaudium et spes; Neno la Mungu: Dei Verbum, Fumbo la Kanisa, Lumen gentium; Ad gentes. Askofu mkuu mstaafu Odongo katika mahojiano maalum na Padre Healey anasema kwamba, Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wote walitia mkwaju hati hizi, kwa ari na moyo wa mshikamano wa Kanisa, wakajiwekea dhamana ya utekelezaji wa Mafundisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika Makanisa mahalia.
Padre Joseph Healey, mmissionari na mwandishi wa vitabu aliyebobea katika tasnia ya habari, alikuwa ni Katibu wa kwanza wa Idara ya Habari, Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA, yenye makao makuu yake, Jimbo kuu la Nairobi, Kenya. Alibahatika pia kufanya kazi kwa karibu sana na Askofu mkuu James Odongo, alipokuwa Mwenyekiti wa AMECEA kuanzia mwaka 1973 hadi mwaka 1979, umri wa mtu mzima kabisa. Hapa ukawa ni mwanzo wa ujenzi wa Jumuiya Ndogo ndogo za Kikristo kama sehemu ya mchakato wa ujenzi wa Kanisa katika Nchi za AMECEA.
Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo zikapania kuwa ni mahali pa kusoma na kulitafakari Neno la Mungu; mahali pa kujiandaa kikamilifu katika maisha ya Kisakramenti sanjari na kumwilisha imani katika matendo ya huruma. Mababa wa AMECEA walikazia pamoja na mambo mengine, umuhimu wa Kanisa mahalia kujitegemea, kujiendeleza na kusimama kwa miguu yake.
Kunako mwaka 1974 hadi mwaka 1975 chini ya uongozi wa Askofu Vincent McCauley, ujenzi wa Makao makuu ya AMECEA ukaanza Jijini Nairobi. Kunako mwaka 1975, AMECEA ikaanzisha kozi maaum ya uhasibu, Chuo cha maendeleo ya jamii, Nyegezi, Jimbo kuu la Mwanza ambacho kwa sasa ni Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino cha Tanzania, SAUT. Mwaka 1976, utume kwa jamii za kichungaji ukaanzishwa na AMECEA. Historia inaonesha kwamba, Kanisa Katoliki katika nchi za AMECEA linaendelea kuimarishwa kwa uwepo wa Jumuiya Ndogo ndogo za Kikristo. Waswahili wanasema, usione vinaelea, kumbuka kwamba, vimeundwa!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.