2015-02-20 09:42:04

Dumisheni amani!


Askofu mkuu Paulino Lukudu Loro, wa Jimbo kuu la Juba, Sudan ya Kusini, anawataka viongozi wa kisiasa nchini humo kuhakikisha kwamba, wanajikita katika mchakato wa ujenzi wa haki, amani na upatanisho wa kitaifa kama suluhu ya kuhitimisha vita ya wenyewe kwa wenyewe iliyolipuka tena nchini humo zaidi ya mwaka mmoja uliopita. Ikiwa kama vita hii haitaweza kusitishwa haraka iwezekanavyo, taifa la Sudan ya Kusini linaweza kuangamia.

Askofu mkuu Paolino Lukudu Loro anawataka wananchi wote kutoka Sudan ya Kusini, kujielekeza zaidi na zaidi katika kujenga na kudumisha umoja na mshikamano wa kitaifa kwa kuondokana na ukabila ambao kwa sasa umepitwa na wakati, kwani hiki kimekuwa ni kikwazo cha ustawi, maendeleo na mafao ya wengi.

Inasikitisha kuona kwamba, maombi yanayotolewa na viongozi wa kidini ili kusitisha vita na kinzani za kijamii mara nyingi yanagonga mwamba, lakini ikumbukwe kwamba, waathirika wakubwa ni wananchi wa kawaida kwani viongozi wa kisiasa wataendelea kupata posho za vikao na kuishi vizuri, huku wananchi wakiendelea kuteseka. Wananchi watambue kwamba, vita bado inapamba moto huko Sudan ya Kusini.

Wakati huo huo, Askofu Edward Hiiboro Kusala wa Jimbo Katoliki Tombura-Yambiro, Sudan ya Kusini anasema, uamuzi wa Serikali wa kuahirisha zoezi la uchaguzi mkuu uliokuwa unapaswa kufanyika mwezi Juni mwaka huu ni wa kishujaa na unapaswa kupongezwa na wapenda amani na maendeleo.

Hivi karibuni, Baraza la Maaskofu Katoliki Sudan ya Kusini katika mkutano wao uliofanyika hivi karibuni walikuwa wameonya kwamba, kusingekuwepo na mafanikio makubwa katika mchakato wa uchaguzi kama ungefanyika mwezi Juni. Kwa sasa, sensa ya watu na makazi inaweza kuendelea na kuwa wabunge wataendelea kumalizia mchakato wa Marekebisho ya Katiba ya Nchi, ili kujipanga vyema kukabiliana na changamoto za kipindi cha mpito.

Ikiwa kama mambo yote haya yatatekelezwa kikamilifu, basi hapana shaka kwamba, uchaguzi mkuu unaweza kufanyika katika mazingira ya haki, amani na utulivu. Maaskofu Katoliki Sudan ya Kusini wanawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusali na kuendeleza amani na utulivu nchini mwao.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.