2015-02-19 10:00:50

Ushindwe na kulegea!


Mzalendo ni mzawa anayependa pahala au nchi yake na yuko tayari kutetea hata kufa. Mwananchi mvunjanchi huyo ni msaliti. Usemi wa zamani wa “mvunjanchi ni mwananchi” unamhusu mzawa asiyekuwa na uzalendo kwa nchi yake. Usemi wa kisasa “Uzalendo umenishinda” unatumika sana na waswahili wanaposhindwa kuutetea uzalendo wao, yaani kuishi itakiwavyo, au hasahasa kutetea ukweli.

Tungeweza kusema pale mtu anaposhindwa kuishi kadiri ya utu wa maisha yake. Mathalani mtu wa ndoa anapovunja uaminifu kwa ndoa yake anajituliza “uzalendo umenishinda”. Maana yake ameshindwa kutetea maadili ya utu wa wito wake au uzalendo kwa ndoa yake. Zamani mtu wa namna hii alijitetea na kusema: “Shetani amenidanganya”. Shetani maana yake mpinzani, mhaini, msaliti, mdanganyifu, mwasi. Kutokana na maana hizi shetani anaonekana kwa macho, kwa vile msaliti huyo, au mvunjanchi na mkosa uzalendo ni wewe mwenyewe hasa pale unapokiri na kusema “Uzalendo umenishinda”.

Ndugu zangu katika biblia kuna nyakati nyingi sana shetani anapoonekana kuwa mhaini, msaliti, mshtaki, mdanganyifu, mwasi na kuwavunjisha watu uzalendo katika maisha yao. Kwa mfano tukimwacha yule shetani aliyemdanganya Eva, yuko shetani yule aliyemsaliti au kumchongea Ayubu kwa Mungu. “Ilikuwa siku moja ambayo hao wana wa Mungu walikwenda kujihudhurisha mbele za Bwana, Shetani naye akaenda kati yao. Alipoulizwa na Mungu ametoka wapi, akajibu “Natoka katika kuzungukazunguka duniani na katika kutembea huku na huku.

Kisha Bwana akamwuliza shetani, “Je, umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu ni mtu mkamilifu…. Ndipo shetani akamjibu Bwana, na kusema, “Je, huyo Ayubu yuamcha Bwana bure?...Nyosha mkono wako sasa uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.” (Ayubu 1:6-11). Yaonekana shetani alikuwa na fursa ya kwenda kwa Mungu akijichanganyachanganya na wenye haki, na huko akawa anatuchongea au kutushtaki kwa Mungu.

Yesu alipokuwa hapa duniani “uzalendo haukumshinda” bali yeye alidumu kuwa mwaminifu kwa Baba yake, licha ya kwamba alizingirwa na mashetani au wasaliti wengi waliotaka kumpotosha asiwe mwaminifu kwa uzalendo aliotumwa kuuishi hapa duniani.

Kwa bahati nzuri wachongezi na wasaliti hao yaani shetani hawana nafasi tena. Shetani ametupwa, hayuko tena mbinguni. Hawezi tena kujichanganya na wengine kwenda kutushtaki kwa Mungu. Nyoka wa agano la kale, yule aliyekuwa anatushtaki asubuhi na jioni kwa Mungu amefukuzwa mbinguni. Yesu alisema, niliona shetani akishuka toka mbinguni kama radi, pale waliporudi wafuasi wale sabini kwa furaha wakisema “Bwana, hata pepo wanatutii kwa jina lako, Yesu akawaambia ‘Nilimwona Shetani akianguka kutokana mbinguni kama umeme’ (Lk. 10:17-18).

Sasa mashetani tunayo hapahapa duniani. Wayahudi waliwaita wapinzani wao Wapersia kuwa ni mashetani. Tunaona katika Injili Yesu anamwita Petro kuwa shetani, “Nenda nyuma yangu, shetani, maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu” (Mk. 8:33). Watu walio na fikra za kibinadamu na siyo za Mungu wanaitwa mashetani. Kadhalika watu wanaotaka kuendeleza ufalme wao wa ukandamizaji, wa kudhulumu wengine hao ni ushetani.

Wainjili Mateo na Luka wanasimulia kirefu na kwa mapana jinsi shetani alivyotaka kumsaliti Yesu kwa kumpa vishawishi vitatu kule jangwani. Mosi kugeuza mawe kuwa mikate, pili kumsujudia shetani ili kupata ufahari, tatu kujitupa toka mnara wa hekalu ili kudakwa na malaika. Mwaka huu tunapata masimulizi ya vishawishi hivyo toka Injili ya Marko katika aya mbili tu. Yatubidi tuzitafakari aya hizo kwa kina sana ili kuweza kupata ujumbe kwa maisha yetu, kwani “Mwenzako akinyolewa wewe tia maji.”

Tunaambiwa: “Mara Roho akamtoa aende nyikani. Akawako huko jangwani siku arobaini, hali akijaribiwa na shetani;” Inashangaza sana kumwona Roho wa Mungu anamsukumia Yesu jangwani ili akashawishiwe, kwa sababu katika sala aliyotufundisha Yesu mwenyewe, tunamwomba Mungu Baba yetu “Usitutie katika kishwawishi.” Hapa yaonekana wazi kwamba Yesu hakupendelewa kwa namna ya pekee, katika maisha haya bali alipitia vishawishi na matatizo kama binadamu wengine nguvu za shetani zilitafuta kumpotosha kutoka uzalendo na maisha ya utu.

Ndiyo maana neno la kigiriki peirazomenos maana yake kuwekwa kiti moto au kujaribiwa. Wayahudi walikaa jangwani miaka jangwani siku arobaini walipotoka huko wakawa washindi. Kwa hiyo jangwani ni mazingira yanayompa mtu fursa ya kukabiliana na shetani ili aweze kuchukua maamuzi mazito ya kuishi uzalendo au kukubali kwamba “uzalendo umemshinda.”

Namba hiyo arobaini ni fumbo na inamainisha maisha yote ya binadamu. Maisha hayo yaweza hata kuwa siku chache tu za kuishi, kama ilivyo usemi wa kiswahili “siku za mwizi ni arobaini”, haimaanishi mwizi anakamatwa zifikapo siku hizo kwani mwizi mwingine hashikwi hadi uzeeni, lakini akikamatwa cha moto atakiona! Kadhalika shetani, ni kitu chochote kile kinachotufanya tuwe mbali na Mungu, kwa hiyo budi tukifahamu sawasawa jinsi kilivyo, kwa sababu kinachukua umbo la mwili, hivi tunaweza kupambana nacho uso kwa uso.

Tunaambiwa tena kuwa kule jangwani Yesu, “alikuwa pamoja na wanyama wa mwitu, na malaika walikuwa wanamhudumia.” Wanyama hao siyo wale tunaowasikia katika kitabu cha Isaya kwamba katika ulimwengu ujao watu wataishi kwa amani na wanyama, la hasha bali ni wanyama wale tunaowasikia katika kitabu cha Daniele, yaani wanyama wanaowakilisha watawala kafiri ambao simba aliyewakilisha wafalme wa Babiloni, dubu aliyewakilisha Wamedi na chui aliwakilisha Wapersia.

Watawala wenye mamlaka wa ulimwengu huu na washawishi wa mambo ya kisiasa. Wakati wa Yesu wanyama hao walilinganishwa na walimu wakuu, Makuhani, Wafarisayo, Masadukao wenye mamlaka ya uchumi, Waandishi wanaohubiri vyema lakini wanashambulia nyumba za wajane na makuhani wanamhubiri Mungu vizuri lakini hawakuyaishi maadili mema ya haki na upendo. Yesu ilimbidi apambane hasa na wanyama kama hawa. Tujihadhari sana tusiwe sisi hao wanyama wakali.

Hatimaye, tunawakuta “malaika walikuwa wakimhudumia”, Hapa malaika haina maana ya kiroho, bali kila mwakilishi aliye chombo cha utumishi wa Mungu kwa ajili ya kuhudumia binadamu. Tunaposema “wewe ni malaika”, hata Musa aliitwa Malaika, kadhalika Yohane Mbatizaji aliitwa pia malaika. Yaani watu wale wanaojituma kumwakilisha Mungu na kufanya matendo mema na mazuri kwa binadamu wenzao kwa jina lake.

Mathalani malaika wa kwanza wa Yesu walikuwa ni Maria na Yosefu, halafu wakafuata watu wengine waliomtumikia na kumwenzi kufanya kazi ya Mungu. Leo kuna malaika wengi wakristu, wanaomtangaza Kristu hasa wanaoituliza mioyo ya waliopondeka na kuwahurumia wengine.

Ndugu zangu, maisha yetu hapa duniani ni kama miaka arobaini, na kuna wanyama na malaika. Tusikubali kuwa wanyama na kusema “uzalendo umenishinda” bali tuwe malaika wema wa kuhubiri Injili ya haki, amani na upendo. “Baada ya Yohana kutiwa gerezani, Yesu akaenda Galilaya, akiihubiri Habari njema ya Mungu akisema wakati umetimia na ufalme wa Mungu umekaribia. Tubuni na kuiamini Injili” (Mk. 1:14-15). Huu ndiyo mwaliko kwetu wakati huu wa Kwaresima.

Na Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.