Baraza la Maaskofu Katoliki Canada katika Kipindi hiki cha Kwaresima linaendesha Kampeni
dhidi ya baa la njaa na utapiamlo ambalo limekuwa ni chanzo kikuu cha maafa kwa watu
kutoka sehemu mbali mbali za dunia, licha ya uzalishaji na uwepo mkubwa wa chakula
duniani, hapa tatizo ni uchoyo na ubinafsi unaojikita katika utamaduni wa watu kutoguswa
na shida pamoja na mahangaiko ya watu wengine duniani. Utu na heshima ya mtu imewekwa
rehani na badala yake, fedha, mali na faida kubwa vimepewa kipaumbele cha pekee.
Kampeni
ya Baraza la Maaskofu Katoliki Canada dhidi ya baa la njaa na utapiamlo wa kutisha
duniani, inasimamiwa na Tume ya Maendeleo na Haki ya Baraza la Maaskofu Katoliki
Canada kwa kuungana na Kampeni iliyozinduliwa kunako mwaka 2013 na Shirikisho la Mashirika
ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationali kwa kuongozwa na kauli
mbiu "familia moja ya binadamu, chakula kwa wote".
Hapa Maaskofu wanawaalika
waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanaonesha ushuhuda wa
imani katika matendo, kwa kujali na kuguswa na mahangaiko ya watu wanaoteseka kwa
baa la njaa duniani. Lengo ni kuwajengea uwezo waamini kujisadaka, ili kugawana matunda
ya kazi ya mikono yao na wasiokuwa na kitu, yaani "akina yakhe pangu pakavu tia mchuzi".
Baraza
la Maaskofu katika ujumbe wake wa Kwaresima kwa mwaka huu linabainisha kwamba, kuna
haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kujifunga kibwebwe ili kupambana na mambo yale yanayosababisha
umaskini wa hali na kipato kwa watu takribani billioni moja. Ikumbukwe kwamba, chanzo
kikubwa cha umaskini ni ukosefu wa haki, mambo yanayochagia pia kutoweka kwa misingi
ya amani na utulivu.
Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linapenda kujielekeza
zaidi na zaidi kwa kugharimia mchakato wa mapambano dhidi ya baa la njaa duniani katika
nchi thelathini, ili kuleta maboresho ya maisha kwa wananchi. Waamini na watu wote
wenye mapenzi mema wanapaswa kutambua kwamba, umaskini unapata chimbuko lake katika
mazingira ambamo hakuna haki, kumbe, haya ni mambo yanayopaswa kuvaliwa njuga na waamini
pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, ili haki ipatikane, amani na utulivu vitawale.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Canada katika ujumbe wake wa Kwaresima, linawaalika waamini kupandikiza
mbegu ya upendo na mshikamano na watu wanaoteseka kwa baa la njaa kwa kuwashirikisha
mapendo na matumaini katika imani inayomwilishwa katika matendo ya huruma. Kwaresima
kiwe ni kipindi cha kufanya tafakari ya kina kuhusu mahusiano ya mtu binafsi na Muumba
wake, bila kuwasahau jirani walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Baraza la Maaskofu
Katoliki Canada linawaalika waamini na atu wote wenye mapenzi mema kupandikiza mbegu
ya mapendo kwa kuchangia kwa hali na mali katika kampeni ya Kwaresima kwa Mwaka 2015.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.