2015-02-19 09:11:15

Hudumieni kwa upendo na ukarimu!


Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil katika kipindi cha Kwaresima mwaka huu sanjari na maadhimisho ya siku ya 52 ya Kampeni ya udugu na mshikamano, limeamua kujikita katika mambo makuu mawili yaani: Kanisa na Jamii kama sehemu ya kauli mbiu ya kipindi cha Kwaresima, kinachowachangamotisha waamini kwa namna ya pekee kujenga na kudumisha upendo na mshikamano wa kidugu. RealAudioMP3
Waamini wanakumbushwa kwamba, Yesu Kristo alikuja hapa duniani si kuhudumiwa, bali kuhudumia na kuyamimina maisha yake ili yaweze kuwa ni fidia ya wengi. Jumatano ya Majivu, iwe ni siku ya kuwakumbusha Wakristo, wito na utume wao na umuhimu wa Jumuiya za waamini kujenga na kudumisha mchakato wa majadiliano katika ukweli na uwazi na jamii inayowazunguka, changamoto iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.
Waamini wanakumbushwa kwamba, wako ulimwenguni kwa ajili ya kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha unaojikita katika haki, amani na maridhiano kati ya watu. Ni changamoto ya kuhakikisha kwamba, wanazingatia utawala wa sheria, kwa ajili ya ustawi, maendeleo na mafao ya wengi.
Kipindi cha Kwaresima, wanasema Maaskofu Katoliki Brazil kwamba, ni muda muafaka wa kujikumbusha kwa mara nyingine tena Nyaraka za Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican; mafundisho yanayolitaka Kanisa kushiriki kikamilifu katika maisha ya watu duniani: Liwe ni Kanisa linalofariji na kuonesha huruma kama ilivyokuwa kwa yule Msamaria mwema. Wananchi wote wanaounda jamii ya Brazil, ni watoto wateule wa Mungu.
Kumbe, ni wajibu wa Wakristo kuhakikisha kwamba, kwa njia ya ushiriki wao wanasaidia mchakato wa maboresho ya miundo mbinu, sheria na mashirika ya kijamii, ili yaweze kuwa kweli ni kwa ajili ya huduma kwa binadamu, ustawi na mafao ya wengi.
Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil, katika ujumbe wake wa Kampeni ya upendo na udugu, linafafanua kwa kina na mapana: historia ya uhusiano kati ya Kanisa na Jamii ya Brazil; hali ya Brazil kwa sasa na changamoto zake. Maaskofu wanaangalia huduma ya upendo na mshikamano inayotolewa na Kanisa Katoliki nchini Brazil; mwingiliano na tofauti kati ya Kanisa na Jamii.
Sehemu ya pili ya tafakari hii ambayo kimsingi ni mwongozo wa Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil, inafafanua mahusiano kati ya Kanisa na Jamii mintarafu mwanga wa Neno la Mungu, Mafundisho ya Mababa wa Kanisa pamoja na Mafundisho Jamii ya Kanisa.
Sehemu ya tatu, Maaskofu wanaipembua jamii ya Brazil mintarafu huduma, majadiliano na ushirikiano kati ya Kanisa na Jamii kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu, heshima, mafao ya wengi na haki jamii. Maaskofu wanatoa vielelezo makini vinavyoweza kutumika kwa ajili ya kumwilisha ujumbe wa upendo na mshikamano wa kidugu wakati wa Kipindi cha Kwaresima kwa mwaka huu.
Mwishoni, Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil, linaonesha mafanikio yaliyopatikana kwenye Kampeni ya mshikamano wa upendo na udugu kwa mwaka 2014 pamoja na miradi iliyotekelezwa kama kielelezo cha ukweli na uwazi katika matumizi ya fedha ya Kanisa inayolenga kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Kunako Mwaka 2016, kutafanyika mshikamano wa upendo na udugu wa kiekumene, kwa kutambua kwamba, kama Wakristo ni wamoja na huo ni wajibu wao. Hii itakuwa ni mara ya nne kwa Baraza la Makanisa nchini Brazil kuandaa kampeni ya kiekumene.
Hii ni kampeni ambayo italishirikisha Shirika la Misaada la Baraza la Maaskofu Katoliki Ujerumani, “Misereor”, ambalo kwa miaka mingi limekuwa mstari wa mbele katika kugharimia miradi ya maendeleo: Barani Afrika, Asia na Amerika ya Kusini. Lengo ni kukuza na kudumisha mchakato wa maendeleo endelevu kwa ajili ya kuboresha huduma ya afya na utu wa kila binadamu. Kwa mara ya kwanza kampeni hii iliendeshwa kunako mwaka 2000, kwa kuongozwa na kauli mbiu “Utu wa binadamu na amani”.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.