2015-02-18 14:50:21

Udugu unavuka mipaka ya rangi, lugha na tamaduni!


Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi, Jumatano tarehe 18 Februari 2015 ameendelea kujikita katika Familia, baada ya kupambanua kwa kina na mapana nafasi na dhamana ya Mama, Baba na Watoto katika maisha na utume wa familia, Baba Mtakatifu ameendelea kufafanua umuhimu wa kudumisha udugu katika familia, neno ambalo lina maana ya pekee katika Ukristo sanjari na historia ya Ukombozi.

Baba Mtakatifu anasema, udugu unaoundwa na kaka na dada katika familia ni uzoefu na mang'amuzi ya kibinadamu ambayo kwa namna ya pekee yanapata mwangwi wake katika maisha ya Yesu Kristo aliyediriki kuwaita ndugu zake, kwani wote ni watoto wa Mungu Baba Mwenyezi. Historia ya Kaini na Abeli inadhihirisha kwamba, kila mtu anapaswa kuwa ni mlinzi na msimamizi wa ndugu yake katika mfumo wa Familia ya binadamu.

Baba Mtakatifu anasema, ndani ya Familia watu wanajifunza kuwa ni watu wema; na kwamba, kile ambacho mtu anajifunza kutoka katika familia yake nyumbani kinakuwa ni chimbuko la utajiri mkubwa kwa jamii katika ujumla wake. Neema ya Kristo inawawezesha waamini kuwaona watu wengine kuwa ni Kaka na Dada, kwa kupatanisha tofauti na kinzani ili kujenga matumaini ya Jamii inayosimikwa katika uhuru na usawa.

Upendo wa kidugu unajionesha kwa namna ya pekee kabisa kwa njia ya huduma kwa watoto wenye matatizo maalum. Yesu anawafundisha wafuasi wake kutambua kwamba, wanapaswa kuwaonesha watu wote upendo, lakini kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa wahitaji zaidi. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, jamii zitaweza kujifunza kujenga na kudumisha moyo wa udugu na kwamba, familia sehemu mbali mbali za dunia zitaweza kufurahia baraka kuu kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayojionesha kwa vijana wanaopenda na kupendwa kama ndugu wamoja.

Mara baada ya Katekesi yake, Baba Mtakatifu Francisko kwa mara nyingine tena, amewaomba waamini na mahujaji waliokuwa wamefika mjini Roma kusikiliza Katekesi yake, kusali kwa ajili ya kuwaombea ndugu zao Wakristo kutoka Misri, waliouwawa kikatili hivi karibuni nchini Libia kwa vile tu, walikuwa ni Wakristo. Baba Mtakatifu anawaombea ili Mwenyezi Mungu aweze kuwapokea katika makao yake ya milele pamoja na kuendelea kuwafariji ndugu na jamaa walioguswa na msiba huu mzito.

Baba Mtakatifu pia anaendelea kuwataka waamini kusali kwa ajili ya kuombea haki na amani huko Mashariki ya Kati na Afrika ya Kaskazini kwa kuwakumbuka marehemu wote, waliojeruhiwa pamoja na wakimbizi. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, Jumuiya ya Kimataifa itaweza kupata suluhu ya amani huko Libya, ambayo kwa sasa imegeuka kuwa ni uwanja wa fujo!

Baba Mtakatifu Francisko akiwasalimia waamini na mahujaji kutoka Mashariki ya Kati amewaambia kwamba, kwa njia ya Fumbo la Umwilisho, uzoefu na mang'amuzi ya udugu katika maisha ya binadamu, waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuwaonjesha watu wote ukarimu, lakini zaidi kwa maskini na wahitaji zaidi.

Yesu ameanzisha udugu unaovuka mipaka ya: rangi, lugha na tamaduni kwa kuwakumbatia wote, kiasi cha kumwita Mwenyezi Mungu, Baba Yetu. Baba Mtakatifu anawataka waamini kukuza na kuimarisha urafiki na mshikamano katika maisha na utume wa Kanisa: Parokiani na katika maeneo ya kazi; maeneo muhimu sana katika kujenga na kudumisha udugu unaojikita katika upendo wa Kiinjili, sadaka na mshikamano wa dhati.

Baba Mtakatifu ameombea pia amani nchini Ukraini na kutambua uwepo wa Watawa wa Shirika la Moyo Mtakatifu wa Yesu kwa ajili ya Katekesi vijijini kutoka Zambia. Amewakumbuka pia wanashirika wa Uamsho wa Kikristo kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaoungana kwa pamoja kwa ajili ya Ibada ya Kuabudu Ekaridti Takatifu, anawahimiza vijana wa kizazi kipya kujitahidi kwenda kukutana na Yesu. Kwaresima ni kipindi maalum anasema Baba Mtakatifu kwa ajili ya kuimarisha maisha ya kiroho, kwa kufunga na kusali; kwa kutawala na kudhibiti vilema katika maisha.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.