2015-02-18 09:00:35

Neno la Mungu!


Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa hapo tarehe 19 Februari 2015, kukutana na kuzungumza na Wakleri kutoka Jimbo kuu la Roma kuhusu umuhimu wa mahubiri katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, chanzo na kilele cha maisha na utume wa Kanisa. Baba Mtakatifu atatoa tafakari na baadaye atawaalika Wakleri kuuliza maswali ili kuondoa duku duku katika miyo yao anasema Kardinali Agostino Vallini, Makamu Askofu wa Jimbo kuu la Roma katika barua aliyowaandikia Wakleri wa Jimbo kuu la Roma. RealAudioMP3
Hii ni fursa kwa Baba Mtakatifu kukutana na kuzungumza na Wakleri wa Jimbo kuu la Roma, walau mara moja kwa mwaka, kadiri ratiba na shughuli za kichungaji zinavyoruhusu, kwani huu ni muda muafaka wa furaha na matumaini mapya katika maisha na utume wa Kanisa.
Mahubiri katika Ibada ya Misa Takatifu ni kati ya mada ambazo Baba Mtakatifu anapenda kuzipatia kipaumbele cha pekee, ili kuwaandaa waamini kuyafahamu Mafumbo ya Kanisa, tayari kujisadaka na kuyatolea ushuhuda kama kielelezo cha imani tendaji, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini. Mambo haya yanafafanuliwa vyema na Baba Mtakatifu mwenyewe katika Waraka wake wa kichungaji, Injili ya Furaha.
Kiongozi wa Ibada hana budi kuonesha moyo wa ibada na unyenyekevu mkuu wakati wa kuadhimisha Mafumbo uya Kanisa, ili aweze kuwashirikisha na kuwamegea waamini, kile ambacho ni matunda ya ukomavu wa imani inayorutubishwa kwa Neno la Mungu na Sakramenti za Kanisa bila kusahau matendo ya huruma. Mahubiri ni sanaa inayobubujika kutoka katika moyo wa sala na ibada, kwa kutambua kwamba, Kiongozi wa Ibada anamwakilisha Yesu Kristo ambaye ndiye kiongozi mkuu anayependa kuwalisha watu wake kwa Neno la Sakramenti.
Baba Mtakatifu Francisko anawakumbusha Wakleri kwamba, maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu si tendo la huruma bali ni haki kwa Familia ya Mungu. Kumbe, mahubiri, si swala la kusoma, bali ni sanaa ya kutangaza Neno la Mungu, linalotafakariwa katika hali ya sala na ukimya, ili kumwachia nafasi Mwenyezi Mungu aweze kuzungumza na waja wake kutoka katika sakafu za mioyo yao. Kiongozi wa Ibada atambue kwamba, Altare si mahali pa kufanyia mchezo wa kuigiza wala uwanja wa kisiasa, bali ni mahali pa sala na sadaka inayopaswa kuadhimishwa kikamilifu ili Mungu aweze kutukuzwa na mwanadamu atakatifuzwe.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.