2015-02-17 10:00:30

Kituo cha kulinda watoto wadogo!


Chuo kikuu cha Kipapa cha Gregorian kilichoko mjini Roma, Jumatatu tarehe 16 Februari 2015 kimezindua Kituo maalum kwa ajili ya kulinda watoto. Baba Mtakatifu Francisko katika tukio hili, amemtumia ujumbe wa matashi mema, Padre Hans Zollner pamoja na wafanyakazi wote wanaojisadaka kwa jili ya ulinzi, malezi na makuzi bora ya watoto dhidi y anyanyaso za kijinsia.

Baba Mtakatifu anawashukuru na kuwapongeza wote kutoka katika undani wa moyo wake. Ni matumaini yake kwamba, kazi hii njema itaweza kuzaa matunda yanayokusudiwa kwa wakati wake. Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuwaombea na kuwaweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria na anawaomba wao pia kumsindikiza kwa njia ya sala katika maisha na utume wake.

Itakumbukwa kwamba, hivi karibuni, Tume ya Kipapa ya ulinzi kwa watoto imehitimisha mkutano wake wa kwanza kwa kukazia umuhimu kwa viongozi wa Kanisa kuhakikisha kwamba, wanaunda mazingira bora na salama kwa makuzi ya watoto. Kutokana na unyeti wa suala lenyewe, wajibu huu unapaswa kutekelezwa kwa makini kwa kuzingatia sheria, kanuni na misingi bora ya maadili.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.