2015-02-15 13:57:28

Gusweni na upendo wa Mungu!


Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, mara baada ya kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na Makardinali wapya, Jumapili tarehe15 Februari 2015, akiwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican anasema kwamba, Mwinjili Marko katika majuma kadhaa anamwosha Yesu anayewaokoa wagonjwa wa kiroho na kimwili; Yesu anayepambana na Pepo wachafu, Yesu anayeshinda nguvu ya giza mahali popote pale anapopita na kupewa nafasi!

Baba Mtakatifu Francisko anasema, wagonjwa wa Ukoma walikuwa wanatengwa na jamii, lakini mgonjwa wa Ukoma baada ya kumwomba Yesu, anaponywa kwa kuoneshwa na kuguswa na huruma pamoja na upendo wa Mungu, kielelezo kwamba, upendo wa Mungu unavuka vizingiti vyote vya maisha. Yesu kwa njia ya ubinadamu wake, ameamua kujitwika magonjwa na mahangaiko ya binadamu, ili aweze kuwakomboa, changamoto na mwaliko kwa waamini kukimbilia huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho.

Kwa njia ya Fumbo la Umwilisho, Mwenyezi Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo anajitwalia hali ya ubinadamu, anateseka hadi kufa Msalabani, ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti na kwamba, Yesu anapambana na dhambi kwa nguvu ya upendo na huruma ya Mungu. Ili waamini waweze kuwa kweli ni wafuasi amini wa Yesu hawana budi kuungana kikamilifu na Yesu mwenyewe, ili kuwa ni vyombo vya upendo na huruma yake, kwa wagonjwa, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Waamini wanahamasishwa kujiachilia ili waguswe na kuambukizwa upendo wa Mungu.

Mwishoni mwa Sala ya Malaika wa Bwana, Baba Mtakatifu amewakumbuka watu kutoka Mashariki wanaojiandaa kuadhimisha Mwaka Mpya, siku kuu inayowakirimia furaha, udugu na maisha ya kifamilia; mambo muhimu katika maisha ya kijamii, changamoto ya kukuza na kuendeleza mahusiano mema kati ya watu; kwa kujikita katika heshima, haki na upendo.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu amewakumbuka na kuwaombea mahujaji wote waliofika mjini Vatican ili kuungana na Makardinali wapya walipokuwa wanasimikwa rasmi, Jumamosi na katika Ibada ya Misa Takatifu, Jumapili, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.