2015-02-15 09:13:26

Familia ni moto wa kuotea mbali!


Kardinali Berhaneyesus Demerew Souraphiel, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Addis Ababa Ethiopia na Mwenyekiti wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA anakuwa ni Kardinali wa pili kutoka nchini Ethiopia baada ya Kardinali Paulos Tzadua, aliyefariki dunia kunako mwaka 2003.

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, changamoto kubwa iliyoko mbele ya Kanisa Barani Afrika ni kuhakikisha kwamba linaendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekumene, ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano kati ya watu. Kanisa halina budi kujielekeza zaidi katika kuwaunganisha watu ambao kwa sasa wanasambaratika kutokana na kinzani za kidini, kisiasa na kikabila, mambo ambayo yanakwamisha mchakato wa maendeleo endelevu Barani Afrika na matokeo yake ni chuki, uhasama, rushwa na ufisadi vinatawala miyo ya watu na kusahau mafao ya wengi.

Kardinali Souraphiel anasema kwamba, Wakatoliki nchini Ethiopia ni wachache ikilinganishwa na Waamini wa Kanisa la Kiorthodox, lakini ni waamini ambao wako imara na thabiti katika imani yao. Si watu wanaoweza kuyumbishwa kwa urahisi, kwani wamefundwa wakafundika katika maisha na utume wa Kanisa. Ni watu wanaotambua kwamba, imani ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, inayopaswa kukumbatia, hadi kieleweke kama wanavyosema Waswahili. Waamini ambao wana imani na matumaini kwa Kristo na Kanisa lake. Ni jamii inayoheshimu zawadi ya Uhai na iko tayari daima kutangaza Injili ya Uhai tangu pale mtoto anapotungwa mimba hadi mauti inapomfika mtu kadiri ya mpango wa Mungu

Kardinali Souraphiel anakiri kwamba, kuna makundi makubwa ya vijana yanayohama kutoka Ethiopia kwenda kwenye Nchi za Falme za Kiarabu ili kutafuta fursa za ajira na wengine wanathubutu hata kuhatarisha maisha yao jangwani na baharini ili kutafuta maisha bora zaidi Barani Ulaya, lakini kwa bahati mbaya, wengi wao wanakufa maji hata kabla ya kuona cheche za maisha bora Barani Ulaya. Vijana wanaofaulu kufika Barani Ulaya, wengi wao wanajikuta wakitumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu, jambo linalodhalilisha utu na heshima yao.

Kardinali Souraphiel anasema, Kanisa nchini Ethiopia linaendelea kuwahamasisha wanasiasa na watu wote wenye mapenzi mema, kujikita katika mchakato wa maboresho ya maisha ya watu wao, kwa kuwekeza katika huduma bora za elimu, afya na maendeleo ya jamii; kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu sanjari na mafao ya wengi. Hii ni changamoto kubwa hata kwa Nchi za AMECEA ndiyo maana Kanisa nchini Ethiopia linaendelea kuwekeza katika sekta ya elimu ambayo ni mkombozi wa wengi.

Kwa njia ya elimu bora inayotolewa na Taasisi zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa, vijana wengi wataweza kupata ujuzi na maarifa na hatimaye fursa za ajira. Kwa mtindo huu, vijana wanaweza kuondokana na kishawishi cha kuikimbia nchi yao ili kwenda ughaibuni, ambako wanadhani kuna "asali na maziwa", lakini huko siku hizi "kumejaa mbigili, ni patahiska nguo kuchanika".

Elimu makini inawawezesha vijana kuwa na maadili mema na kuachana na mambo ambayo yanaleta kichefu chefu na simanzi katika maisha ya kijamii. Ukosefu wa fursa za ajira ni changamoto kubwa ambayo haina budi kufanyiwa kazi kwa umakini mkubwa, kwani ukosefu wa fursa za ajira miongoni mwa vijana kuna athari kubwa sana katika kukoleza misingi ya haki, amani na utulivu. Vijana wasiokuwa na ajira mara nyingi wamekuwa wanatumiwa na baadhi ya watu kusababisha kinzani na migawanyiko ya kijamii, kwa kulipwa ujira kiduchu! Elimu inaweza kusaidia kupambana na majanga ya kijamii, kwa kuimarisha maadili mema.

Kardinali Souraphiel anasema kwamba, Familia Barani Afrika inapewa kipaumbele cha kwanza ndiyo maana Kanisa linaendelea kujiwekea sera na mikakati ya kichungaji, ili kuzijengea familia za Kikristo uwezo wa kutangaza kwa njia ya ushuhuda makini wa maisha Injili ya Familia, kwa kuendelea kujikita katika tunu bora za maisha ya ndoa na familia. Kardinali Souraphiel anasema, chezea kwingine, lakini Familia ni moto wa kutoea mbali.

Bado kuna shida na changamoto nyingi zinazozikabili Familia nyingi Barani Afrika, kwa mfano umaskini unaotokana na ukosefu wa fursa za ajira, unaowalazimisha akina baba kuacha familia zao ili kwenda mbali kutafuta riziki ya maisha, kuna changamoto za malezi katika ndoa mseto; kuna uwepo wa familia tenge inayosimamiwa na kuongozwa na mzazi mmoja; kuna magonjwa ambayo yanawaacha watoto wengi wakiwa ni yatima pasi na msaada. Zote hizi ni changamoto kubwa katika maisha na utume wa Familia Barani Afrika.

Ni matumaini ya Familia ya Mungu Barani Afrika kwamba, Sinodi ya Maaskofu kuhusu Familia inayoongozwa na kauli mbiu "Wito na utume wa familia ndani ya Kanisa na ulimwengu mamboleo" itaweza kuibua sera na mikakati ya shughuli za kichungaji katika maisha ya ndoa na familia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.