Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican kwa mamlaka aliyokabidhiwa na Baba
Mtakatifu Francisko, amemteua Mama Mariella Enoc kuwa Rais mpya wa Baraza la Uongozi
wa Hospitali ya Bambino Gesù inayoongozwa na kuendeshwa na Vatican. Rais Mariella
Enoc anachukua nafasi iliyoachwa wazi baada ya Professa Giuseppe Profit, kujiuzuru,
mwezi Januari 2015.
Pamoja na masuala mbali mbali ya uongozi katika Hospitali
ya Bambino Gesù, Rais Mariella Enoc atajihusisha pia ni shughuli za utawala wa kila
siku wa Hospitali hii ambayo imekuwa maarufu sana kutokana na huduma makini kwa watoto
wadogo ndani na nje ya Italia.
Mama Mariella Enoc alizaliwa kunako mwaka 1944
huko Novara, Italia. Kwa sasa ni Makamu wa Rais wa Mfuko wa Cariplo ni mwanamke mwenye
uzoefu mkubwa katika kuendesha na kusimamia shughuli za Hospitali. Kabla ya uteuzi
huu, alikuwa pia ni kati ya wajumbe wa Baraza la Uongozi wa Hospitali ya Bambino Gesù.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.