2015-02-13 14:51:32

Majadiliano ya kidini!


Padre Indunil Kodithuwakku, Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini anaongoza ujumbe wa viongozi wa Baraza hili katika mikutano ya majadiliano ya kidini iliyoanza nchini India, kuanzia tarehe 12 na itahitimishwa hapo tarehe 17 Februari 2015. Askofu mkuu Salvatore Pennacchio, Balozi wa Vatican nchini India anashiriki pia katika matukio haya. Washiriki wa mikutano hii ni kutoka katika nchi mbali mbali za Bara la Asia.

Wabudha na Wakristo katika mchakato wa kudumisha udugu, ndiyo kauli mbiu inayoongoza majadiliano haya kwa kutambua kwamba, binadamu wote kwa pamoja wanaunda familia ya Mungu. Itakumbukwa kwamba, kuna mwingiliano wa tamaduni, lakini kama waamini wanahimizwa kujenga utamaduni wa udugu na mshikamano, ili kwa pamoja waweze kupambana na maovu yanayoendelea kujitokeza ndani ya jamii, kwani mshikamano wa udugu, unafuta machozi na huu ndio mwelekeo mpya.

Haya kimsingi ni mambo makuu ambayo yanaendelea kujadiliwa na wajumbe katika mikutano iliyoandaliwa na Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini huko India kwa kushirikiana na Baraza la Maaskofu Katoliki India. Baraza la Kipapa linaadhimisha Jubilee ya miaka 50 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha Waraka kuhusu majadiliano ya kidini, chombo ambacho kimekuwa mstari wa mbele katika mchakato wa kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani na uhuru wa kidini.







All the contents on this site are copyrighted ©.