2015-02-13 09:08:32

Mageuzi yaliyokwishafanyika!


Baba Mtakatifu Francisko kwa kusoma alama za nyakati amefanya marekebisho makubwa katika mfumo wa fedha na uchumi mjini Vatican kwa kukazia: ukweli, uwazi, uaminifu na uwajibikaji kwa fedha za Kanisa zinazopania kuliwezesha Kanisa kutekeleza utume wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili sanjari na kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.

Mtakatifu Yohane Paulo II katika maisha na utume wake, alifanya mageuzi makubwa katika maisha na utume wa Kanisa kwa kuandika Waraka wa shughuli za kichungaji, maarufu kama "Pastor bonus". Papa akafuta Baraza la Kipapa la majadiliano na wasioamini kwa kuliunganisha na Baraza la Kipapa la Utamaduni. Papa Yohane Paulo II akaunda Tume ya kutunza mambo ya kale, ambayo hapo awali ilikuwa imeunganishwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Wakleri na hapa ikaanza kujulikana kama Tume ya Kipapa kwa ajili ya mambo ya kale ya Kanisa, inayoendelea kushirikiana kwa karibu zaidi na Baraza la Kipapa la Utamaduni.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kunako mwaka 2010 akaunda Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Uinjilishaji Mpya. Mwaka 2011, akaondoa mamlaka ya kutengua uhalali wa Sakramenti ya Daraja Takatifu kutoka kwenye Baraza la Kipapa la Ibada, Nidhamu na Sakramenti za Kanisa na kuanzisha Ofisi ambayo kwa sasa iko katika Mahakama kuu ya Kanisa yaani, Rota Romana. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI aliunganisha pia Tume ya Kipapa ya mambo ya kale ya Kanisa kwenye Baraza la Kipapa la Utamaduni.

Ilikuwa ni mwaka 2013, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI alipoamua kuondoa madaraka yanayohusu Seminari kutoka kwenye Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki na kuyaweka mamlaka haya chini ya Baraza la Kipapa la Wakleri. Masuala ya Katekesi yalihamishwa kutoka kwenye Baraza la Kipapa la Wakleri kwenda kwenye Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Uinjilishaji mpya. Kwa ufupi haya ndiyo mabadiliko makubwa ambayo yamefanywa katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, kwa kusoma alama za nyakati ili kuliwezesha Kanisa kutekeleza utume wake kwa ufanisi mkubwa zaidi.

Na Padre Ricahrd A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.