Umoja wa Mataifa unabainisha kwamba, kuna zaidi ya watoto 250, 000 ambao wamepelekwa
mstari wa mbele kama wapiganaji, hasa katika nchi maskini zaidi duniani. Hawa ni watoto
ambao wamepokwa matumaini ya kupata fursa ya elimu, ili kuwa na matumaini ya kesho
iliyo bora zaidi. Ni kundi la watoto ambalo linafanyishwa kazi za kijeshi au wakati
mwingine wanapigana bega kwa bega na wanajeshi wengine.
Takwimu hizi zimetolewa
na Umoja wa Mataifa, Alhamis, tarehe 12 Februari 2015, Siku ya Kimataifa dhidi ya
ajira ya watoto wadogo jeshini. Shirika la kuhudumia watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF,
linaonesha wasi wasi mkubwa kutokana na taarifa zinazoendelea kuwasili kutoka Sudan
ya Kusini na Jamhuri ya watu wa Afrika ya Kati, zikionesha kwamba, kuna idadi kubwa
ya watoto wanaoandikishwa jeshini, tayari kupelekwa mstari wa mbele kupigana kama
chambo!
Tukio hili limeadhimishwa wakati ambapo Jumuiya ya Kimataifa inafanya
kumbu kumbu ya Protokali ya hiyari kuhusu haki za watoto wadogo na vijana iliyopitishwa
na Umoja wa Mataifa kunako mwaka 2002. Hiki ni chombo cha kisheria ambacho kimetiwa
mkwaju na Nchi 153 ili kuzuia uandikishaji wa watoto wadogo kwenye majeshi au kwa
kuajiriwa kwenye makundi ya wanajeshi waasi.