2015-02-12 09:14:34

Lolote atakalowaambia fanyeni!


Maadhimisho ya Siku za Wagonjwa Duniani ni mwaliko na changamoto kwa waamini kuhakikisha kwamba, wanawasaidia na kuwaonjesha wagonjwa imani, matumaini na mapendo katika hija ya maisha yao, kwa kutambua kwamba, hata katika magonjwa yao, bado utu na heshima yao kama binadamu inapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa na wote!

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kujisadaka kwa njia ya huduma makini kwa wagonjwa, wazee, walemavu na watu pweke, ili waweze kuonja tena thamani na utu wao kama binadamu, walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Kadiri ya taratibu zilizowekwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kwamba, maadhimisho makuu ya Siku za Wagonjwa, Familia na Vijana yatafanyika katika ngazi ya kimataifa kila baada ya miaka mitatu. Kutokana na mantiki hii, Maadhimisho ya Siku ya 24 ya Wagonjwa Duniani kwa Mwaka 2016 yatafanyika mjini Nazareth, Nchi Takatifu, kwa kuongoza na kauli mbiu "Kujiaminisha kwa Yesu kama Bikira Maria: Lolote atakalowaambia fanyeni" (Yoh. 2:5).

Hapa Bikira Maria anakuwa ni kielelezo muhimu cha imani tendaji na faraja kwa wote wanaoteseka kiroho na kimwili pamoja na mshikamano wa upendo na udugu kutoka kwa wahudumu wa sekta ya afya, ndugu na majirani. Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika Sekta ya Afya mwaka 2015 linaadhimisha kumbu kumbu ya miaka thelathini tangu lilipoanzishwa na Mtakatifu Yohane Paulo II. Katika miaka yote hii, limekuwa ni kituo rejea cha imani, matumaini, mapendo na mshikamano katika sekta ya afya, kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu.

Padre Augusto Chendi, Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya anabainisha kwamba, Mwaka 2015, Kanisa linaadhimisha kumbu kumbu ya Miaka 20 tangu Mtakatifu Yohane Paulo II alipochapisha Waraka wa Injili ya Uhai, ili kulisaidia Kanisa kusimama kidete kulinda, kutetea, kuhudumia na kutangaza Injili ya Uhai.

Tarehe 25 Machi 2015, Baraza hili la Kipapa litapembua kwa kina na mapana: matatizo na changamoto zinazojitokeza katika Injili ya Uhai, ili kuwasaidia waamini na watu wenye mapenzi mema, kukataa katu katu utamaduni wa kifo. Tarehe 15 na 16 Mei, 2015 kutafanyika kongamano la kimataifa kuhusu magonjwa nadra katika maisha ya mwanadamu, lengo ni kujenga na kukuza mshikamano wa upendo. Tarehe 18 Mei 2015 wajumbe kutoka Mabaraza ya Maaskofu Katoliki duniani watapanga na kuibua mbinu mkakati wa kupambana na changamoto pamoja na vizingiti dhidi ya Injili ya Uhai.

Baraza linajiandaa pia kuchapisha Mwongozo kwa ajili ya wafanyakazi katika Sekta ya Afya, ili kupyaisha Mwongozo uliokuwa umechapishwa kunako mwaka 1994, ili kutetea Injili ya Uhai kwa kuzingatia kanuni maadili, utu wema na Mafundisho ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.