Baba Mtakatifu Francisko katika mwendelezo wa katekesi yake kuhusu familia baada ya
kuzungumzia: Mama na Baba, Jumatano tarehe 11 Februari 2015 amewageukiwa watoto ambao
ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu; kwa kutambua umuhimu na dhamana yao katika
maisha ya kifamilia. Nabii Isaya anasema inua macho yako, utazame pande zote: wote
wanakusanyana, wanakujia wewe. Wanawako watakuja kutoka mbali, na binti zako watabebwa
nyongani. Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, moyo wako utatetemeka na kukunjuka.
Baba
Mtakatifu anasema, watoto ni chamchemi ya furaha na matumaini kwa wazazi wao; matunda
ya upendo kati ya Baba na Mama na zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu anayemkiria
kila mtu anayezaliwa ulimwenguni hadhi na utu unaopaswa kulindwa na kuheshimiwa.
Amri
ya nne ya Mungu, inawataka watoto kuwaheshimu wazazi na ni mwaliko kwa waamini na
watu wote wenye mapenzi mema kuona mahusiano yaliyopo kati ya vizazi na kifungo cha
Kimungu ambacho kinaathiri mahusiano mengine yote muhimu ndani ya Jamii katika ujumla
wake. Kanisa kwa namna ya pekee linapenda kukazia uwajibikaji na ukarimu wa kurithisha
zawadi ya uhai katika jamii yenye afya bora; inayoimarishwa na kupyaishwa sanjari
na kuboreshwa kwa uwepo wa vijana wa kizazi kipya.
Baba Mtakatifu Francisko
anamwomba Yesu, Mwana wa Mungu na familia ya binadamu, awasaidie waamini na jamii
katika ujumla wake, kulinda na kuthamini zawadi ya uhai; utu na heshima ya familia
sanjari na kutekeleza dhamana ya kuwasaidia vijana wa kizazi kipya kuwa na matumaini,
furaha na ujasiri kwa leo na kesho iliyo bora zaidi.
Baba Mtakatifu anaungana
na mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaofanya hija ya maisha ya kiroho
kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Lourdes, Ufaransa, kutambua umuhimu wa kupokea
na kutunza zawadi ya uhai kwa ukarimu na furaha, ili kujenga na kuimarisha umoja na
udugu. Ulimwengu unawahitaji Wakristo wanaoshuhudia imani yao kwa Mwenyezi Mungu kwa
njia ya ukarimu sanjari na kukumbatia zawadi ya uhai. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu
kwamba, familia zitaendelea kushirikiana kutekeleza mpango wa Mungu katika maisha
yao.
Baba Mtakatifu anasema, watoto ni zawadi ambayo inapaswa kulindwa, kutunzwa
na kuendelezwa kwa hali na mali na wazazi pamoja na walezi. Watoto kwa upande wao,
wanapaswa kuwaheshimu, kuwatunza na kuwasaidia wazazi wao, wote wakiwa wameunganika
katika kifungo cha upendo. Baba Mtakatifu anawaombea watoto wema pamoja na kumwomba
Mwenyezi Mungu ili aweze kuwaongoa watoto watukutu.
Mara baada ya Katekesi
yake, Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, kwa masikitiko makubwa amepokea taarifa
za wahamiaji waliofariki dunia kwenye bahari ya Mediterrania kutokana na baridi kali
wakati wakiwa njiani kuelekea Italia. Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia wahanga
wa tukio hili sala zake pamoja na kuendelea kuhimiza mshikamano, ili asiwepo hata
mtu mmoja anayekosa msaada.
Mwishoni, Baba Mtakatifu anawaalika waamini pamoja
na watu wote wenye mapenzi mema kusali kwa ajili ya kuwaombea Makardinali watakaokutanika
mjini Vatican, ili Roho Mtakatifu awasaidie katika kazi zao na kuwaangazia Makardinali
wapya ili waweze kutekeleza barabara huduma yao kwa Kanisa.
Na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.