Baraza la Kipapa la Ibada, nidhamu na Sakramenti za Kanisa limezindua rasmi Mwongozo
wa Mahubiri, ili kuwasaidia Wakleri kupata sanaa itakayowawezesha kutangaza Habari
Njema ya Wokovu kwa umakini zaidi, kwani mahubiri si mahali pa kuwakaripia watu, wala
jukwaa la michezo ya kuigiza. Tayari Mwongozo huu umekwisha chapishwa na Idara ya
Uchapaji ya Vatican, katika lugha ya Kiingereza na Kiitalia, ili kuyasaidia Mabaraza
ya Maaskofu kufanya tafsiri kwa lugha mbali mbali.
Akizindua Mwongozo huu,
Kardinali Robert Sarah, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Ibada, nidhamu na Sakramenti
za Kanisa, anasema, hiki ni chombo ambacho kimekuwa kikisubiriwa kwa hamu kubwa kutokana
na mahitaji yake msingi, yanayopania kuleta maboresho katika maadhimisho ya Liturujia
ya Kanisa, ili kumtukuza Mwenyezi Mungu na mwanadamu kutakatifuzwa.
Ni changamoto
ambayo ilianza kujitokeza wakati wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu iliyofanyika
kunako mwaka 2005 na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI akakazia umuhimu wa mahubiri
katika Waraka wake wa kitume, Neno la Bwana, "Verbum Domini", kwa kusema kwamba, mahubiri
ni sanaa ambayo Wakleri wanapaswa kujifunza. Papa Francisko katika Waraka wake wa
kitume, Injili ya Furaha, "Evangelii gaudium" anasema, Kanisa halina budi kufanya
maboresho makubwa ili kuwasaidia Wakleri waweze kuhubiri vyema, kwa kutambua kwamba,
wao ni Wahudumu wakuu wa Neno la Mungu.
Hapa anasema Kardinali Sarah, kuna
haja ya kujifunza kuhubiri, ili kuweza kuwasilisha vyema ujumbe unaokusudiwa na Mama
Kanisa kwa ajili ya Familia ya Mungu, kwani mahubiri yanapaswa kuwa ni kielelezo cha
maisha na utume wa Mhubiri, kwani anapaswa kuhubiri kile anachoishi na kutenda. Mkleri
lazima ajitahidi kumhubiri, Mungu aliye hai, jambo ambalo linapata chimbuko lake katika
majadiliano kati ya Mwenyezi Mungu na Padre katika sala na tafakari.
Umuhimu
wa mahubiri, umefafanuliwa kwa kina na mapana na Askofu mkuu Arthur Roche, Katibu
mkuu wa Baraza la Kipapa la Ibada, nidhamu na Sakramenti za Kanisa kwa kusema kwamba,
Wakleri hawana budi kujiandaa kikamilifu kabla ya kuanza kuhubiri, kwani hii ni sehemu
muhimu sana ya utume wao kama Mapadre, changamoto na mwaliko kwa Wakleri kujisadaka
kutafuta muda wa kutosha kwa ajili ya kusali, kutafakari na kuandaa mahubiri mazuri
yanayomwilishwa katika uhalisia wa maisha yao mintarafu changamoto za shughuli za
kichungaji.
Magwiji wa mahubiri kama akina Mtakatifu Ambrose na Papa Leo mkuu
wanabainisha kwamba, mahubiri mazuri ni yale yanayogusa watu kutoka katika undani
wa mioyo yao katika matukio husika na kwa wakati muafaka. Wakleri wasihubiri kiasi
cha kuwachosha watu na kuanza kusinzia na wala wasitoe mahubiri mafupi kana kwamba,
wanaharaka ya kufa mtu! Wakleri wawe makini kusoma alama za nyakati na mazingira.
Kardinali Sarah anasema, kwa maeneo ambayo waamini wanafika mara moja kwa
ajili ya kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu, hapa kuna haja ya kuhakikisha kwamba,
wanapatiwa Neno litakalowasaidia katika hija ya maisha yao; Watu wa Mungu wafundishwe
kikamilifu bila kuwachosha au kuwatesa kwa mahubiri marefu!
Akichangia mada
katika uzinduzi wa Mwongozo wa mahubiri, Padre Filipo Riva, afisa wa Baraza hili la
Kipapa anasema, watu wanachoka kusikiliza mahubiri yasiyokuwa na mashiko na matokeo
yake, wanaanza kusinzia na kukosa hamu ya kushiriki kikamilifu katika maadhimisho
ya Ibada ya Misa Takatifu. Pale inapofaa kuna haja ya kusikiliza shuhuda kutoka kwa
waamini wenyewe, kama sehemu ya mchakato wa sanaa ya majadiliano katika maadhimisho
ya Liturujia ya Kanisa.
Mwongozo huu umegawanyika katika sehemu kuu mbili:
Sehemu ya kwanza ni: Mahubiri na Mazingira ya Kiliturujia, hapa Kanisa linatoa maana
ya mahubiri katika maisha na utume wa Kanisa. Sehemu ya Pili inahusu: mbinu, mikakati
na mahudhui ya sanaa ya mahubiri. Mahubiri yazingatie Liturujia ya Kanisa. Mwongozo
wa mahubiri ni chombo kinachopania kuwasaidia Wakleri kuandaa mahubiri kadiri ya Liturujia
ya Kanisa. Maaskofu wa majimbo wanahamasishwa kuhakikisha kwamba, wanasaidia mchakato
wa maboresho ya mahubiri majimboni mwao. Majandokasisi wafundwe barabara sanaa ya
mahubiri, tangu mwanzo wanapokuwa Seminarini.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican