2015-02-10 08:48:48

Wao, Siku ya Wapendanao!


Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani linaadhimisha Juma la Sita Kitaifa kuhusu Ndoa, nafasi ya pekee kwa ajili ya kusherehekea tunu msingi za maisha ya ndoa na familia na baraka inayobubujika katika maisha ya ndoa. Ni fursa kwa Mama Kanisa kuendelea kuwasindikiza wanandoa katika maisha na utume wao, ili kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika maisha yao.

Ni kilele cha upendo wa dhati kati ya bwana na bibi wanaoshikamana hadi kifo kwa njia ya Sakramenti ya Ndoa Takatifu. Kilele cha Juma hili ni hapo tarehe 14 Februari, maarufu kama Siku ya Wapendanao duniani! Maadhimisho ya mwaka huu yana umuhimu wa pekee kwani hii ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Familia Kimataifa itakayoadhimishwa Jimbo kuu la Philadelphia, Marekani sanjari na Sinodi ya Maaskofu kuhusu Familia, itakayofanyika mjini Vatican, mwezi Oktoba, 2015, kwa kuongozwa na mada "Wito na utume wa Familia ndani ya Kanisa na Ulimwengu mamboleo".

Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaadhimisha Juma hili kwa njia ya sala kwa kuwaombea wanandoa, siku ambayo imeadhimishwa nchini Marekani Jumapili tarehe 8 Februari 2015. Maaskofu wamechapisha vitini vinavyoonesha umuhimu wa maisha ya ndoa na familia katika maisha na utume wa Kanisa, changamoto kwa waamini kujikita katika tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, ili kuwatangazia walimwengu Injili ya Familia, kwa njia ya ushuhuda wa maisha.

Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, limechagua tarehe 13 Februari 2015 kuwa ni Siku maalum ya kuombea heshima na utakatifu wa maisha ya ndoa na familia, kadiri ya mpango wa Mungu. Ni Siku ya kufunga na kusali, ili kuomba toba na huruma ya Mungu kwa wanandoa, ili waweze kudumu katika fadhila ya uaminifu hata pale wanapokabiliana na changamoto mbali mbali za maisha. Wanandoa wasikate wala kukatishwa tamaa, bali waendelee kumtumainia Mungu katika maisha yao ya kila siku. Kuna watu wamekwisha adhimisha Jubilee ya Miaka 50 ya Ndoa, kumbe, hili ni jambo linalowezekana kwa msaada na neema ya Mungu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.