2015-02-10 09:37:35

Uchaguzi mkuu Nigeria, kitendawili!


Askofu mkuu Ignatius Ayau Kaigama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria anasema kwamba, wananchi wengi hawakufurahia na uamuzi uliofanywa na Tume Huru ya Uchaguzi nchini Nigeria wa kuamua kuhairisha uchaguzi mkuu hadi tarehe 28 Machi 2015 kutokana na sababu za kiusalama.

Uchaguzi mkuu nchini Nigeria ulikuwa umepangwa kufanyika tarehe 14 Februari 2015. Wachunguzi wa mambo wanasema, kama Serikali imeshindwa kudhibiti vitendo vya kigaidi vinavyofanywa na Kikundi cha Boko Haram, siku hizi chache, itakuwa imepata wapi jeuri ya kulinda raia na mali zao?

Askofu mkuu Kaigama anatumaini kwamba, uamuzi huu umefikiwa kwa ajili ya mafao ya wengi nchini Nigeria na kwamba, Kanisa Katoliki nchini humo linaendelea kuwahamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi mkuu, kama sehemu ya utekelezaji wa haki yao msingi kikatiba.

Maaskofu wanawataka wananchi wote wa Nigeria kuzingatia: haki, amani, usalama na utulivu ili kufanikisha zoezi la upigaji kura. Juhudi hizi zinakwenda sanjari na majadiliano ya kidini kama sehemu ya mchakato wa kujenga na kukuza: haki, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa, lengo ni kuhakikisha kwamba, uchaguzi unakuwa huru na wa haki; mambo msingi yatakayosaidia kuchochea maendeleo endelevu nchini Nigeria.

Na Padre Richard A. Mjigwa. C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.