2015-02-10 08:35:44

Kumbu kumbu ya miaka 47 ya huduma kwa maskini!


Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, tarehe 9 Februari 2015 imeadhimisha kumbu kumbu ya miaka 47 tangu ilipoanzishwa kwa Ibada ya Misa Takatifu iliyoadhimishwa na Kardinali Jaime Lucas Ortega Alamino, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Havana, Cuba, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, Jimbo kuu la Roma.

Ibada hii imehudhuriwa na waamini pamoja na viongozi mbali mbali wa Serikali na taasisi za kimataifa. Sala, maskini na amani ni mambo makuu matatu yanayounda dira, mwelekeo na mikakati ya shughuli za kitume zinazotekelezwa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, sehemu mbali mbali za dunia. Jumuiya hii ina jumla ya wanachama 60, 000 wanaotekeleza utume wao katika nchi 73 duniani, wote hawa ni watu wa kujitolea.

Jumuiya ya Mtakatifu Egidio imeendelea kujielekeza zaidi na zaidi katika mchakato wa kutafuta suluhu ya amani katika maeneo ambayo kwa sasa yanazidi kuwaka moto kutokana na vita na kinzani za kijamii na kisiasa. Jumuiya hii pia ni shuhuda wa huduma ya upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.