2015-02-10 08:48:17

Iweni mashuhuda wa Injili ya Familia!


Baraza la Maaskofu Katoliki New Zealand, linawataka waamini kutolea ushuhuda wenye mvuto na mashiko katika maisha ya ndoa na familia katika maeneno wanamoishi na kufanya kazi, ili Watu wa Mataifa waguswe na ujumbe wa Injili ya Familia, inayotangazwa kwa njia ya ushuhuda makini! Changamoto hii ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Familia, itakayoadhimishwa mjini Vatican, mwezi Oktoba 2015.

Baraza la Maaskofu Katoliki New Zealand linasema kwamba, maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu familia ni matunda ya tafakari ya kina, sala, tafiti na mang'amuzi katika maisha na utume wa Kanisa, ili kubainisha sera na mikakati ya shughuli za kichungaji zitakazowasaidia wanandoa kutangaza Injili ya Familia kwa ari na moyo mkuu zaidi, licha ya changamoto na magumu wanayokabiliana nayo kila siku ya maisha yao.

Maaskofu wanakumbushwa kwamba, Sinodi maalum ya Maaskofu iliyofanyika mjini Vatican mwaka 2014, ilijielekeza zaidi katika kupambanua mikakati, sera, dira na maelekeo ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya familia katika ulimwengu mamboleo. Kuna haja kwa waamini kuendelea kujikita katika maboresho ya maisha ya ndoa na familia, kwa njia ya sala, tafakari, Sakramenti za Kanisa; upendo na msamaha; mambo msingi katika udumifu kwenye ndoa. Kwa sasa waamini wanaendelea kuhamasishwa ili kuchangia mawazo, tafakari na mang'amuzi yao, tayari kupelekwa kwenye Sekretarieti kuu ya Sinodi, ili "Hati ya Kutendea Kazi" iweze kuandaliwa.

Baraza la Maaskofu Katoliki New Zealand linawamasisha wanandoa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Mwaliko huu unawaendea hata wale wanaodhani kwamba, Mama Kanisa amewasahau katika maisha na utume wake kutokana na kasoro za maisha ya ndoa na familia. Maaskofu wanawaalika wote hawa kushirikisha mawazo yao, kwani Mchungaji mwema, anapenda kutembea na watoto wake wote, akitambua kwamba, kati yao kuna wale wanaohitaji msaada zaidi.

Maaskofu wanawahimiza waamini kujibu maswali dodoso kadiri ya hali na maisha yao ya ndoa na familia na wala si lazima kujibu maswali yote yaliyoulizwa, kwani Mama Kanisa anapenda kusikiliza sauti ya mwamini mmoja mmoja, ili hatimaye, kufahamu sauti ya Familia ya Mungu nchini New Zealand, kadiri ya mwanga wa Roho Mtakatifu. Majibu yote ya maswali dodoso yanapaswa kuwa yamekwisha kusanywa ifaikapo tarehe 14 Aprili 2015, tayari kwa maandalizi ya Hati ya kutendea kazi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.