Baraza la Maaskofu Katoliki Australia linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi
mema kushikamana kwa dhati katika mapambano dhidi ya utumwa mamboleo na biashara haramu
ya binadamu; mambo ambayo ni uhalifu dhidi ya ubinadamu.
Itakumbukwa kwamba,
kwa mara ya kwanza, Kanisa hapo tarehe 8 Februari 2015, katika maadhimisho ya kumbu
kumbu ya Mtakatifu Josefina Bhakita, mtawa wa Mabinti wa Canossa kutoka Sudan, aliyekombolewa
kutoka utumwani na hatimaye kutangazwa na Papa Yohane Paulo II kunako mwaka 2000,
limeadhimisha Siku ya kwanza ya kimataifa ya kupambana na biashara haramu ya binadamu.
Hii imekuwa ni fursa kwa ajili ya kusali, kutafakari na kuibua mbinu mkakati
wa kupambana na biashara haramu ya binadamu. Baraza la Maaskofu Katoliki katika ujumbe
wao kwa siku hii, wanasema, kamwe binadamu si bidhaa ya kuuzwa sokoni!
Biashara
haramu ya binadamu inaendelea kushamiri sehemu mbali mbali za dunia kwa sababu watu
wenyewe wameamua iendelee, lakini wakiamua kwa kauli moja, biashara haramu ya binadamu
inaweza kukomeshwa na hivyo kuponya madonda makuu yanayowaandama watu zaidi ya millioni
27 kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Hawa ni wanawake, wasichana na watoto wanaonyimwa
uhuru na utu wao unawekwa rehani, kiasi cha kugeuzwa kuwa kama bidhaa sokoni. Kutokana
na watu hawa kudhalilishwa utu na heshima yao, kuna haja ya watu wote wenye mapenzi
mema kusimama kidete kupinga na hatimaye, kukomesha biashara haramu ya binadamu.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Australia, linaialika Jumuiya ya Kimataifa kushikamana kwa dhati,
ili kuhakikisha kwamba, biashara haramu ya binadamu inapewa ufumbuzi wa kudumu. Bado
kuna makundi makubwa ya wanawake, wasichana na watoto yanatumbukizwa katika utumwa
mamboleo; baadhi ya watoto wanafanyishwa kazi za suluba kwenye mashamba makubwa na
kwenye migodi; ni wazalishaji wakubwa viwandani na katika sekta ya uvuvi, lakini wanaishi
na kufanya kazi katika mazingira duni na magumu. Hadi leo hii kuna wasichana 200 kutoka
Nigeria walitekwa nyara na kikundi cha kigaidi cha Boko Haram hadi leo hii hawajulikani
mahali walipofichwa.
Kumbe, kuna haja ya kuzuia uhalifu huu dhidi ya ubinadamu;
kuwalinda wahanga, kuwashughulikia wahusika kadiri ya sheria na kushirikiana kwa ajili
ya kufanya mabadiliko makubwa katika jamii. Hii ni changamoto kubwa inayowashirikisha
watu wote kila mtu kadiri ya nafasi na dhamana yake katika jamii.
Tarehe 8
Februari 2015 ni siku ambayo ilichaguliwa na Baraza la Kipapa la haki na amani kwa
kushirikiana na Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wahamiaji, wakimbizi
na watu wasiokuwa na makazi maalum pamoja na Shirikisho la Mashirika ya Kitawa na
Kazi za Kitume, wameamua kwamba, kuanzia tarehe 8 Februari 2015, siku hii itakuwa
inaadhimishwa na Kanisa lote ulimwenguni Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.