2015-02-07 15:54:56

Zingatieni haki na kutenda mema!


Ujumbe wa Kwaresima kutoka katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kwa mwaka 2015 unaongozwa na kauli mbiu "Zingatieni haki na kutenda mema, (Isa 56:1)

UTANGULIZI:

Wapendwa Taifa la Mungu,
“Neema na iwe kwenu, na amani zitokazo kwa Mungu, Baba yetu” (Kol 1:2). Tunapoanza kipindi cha Kwaresima, kipindi cha toba na uongofu wa nafsi zetu, “tujiandae kuruhusu nafsi zetu zitajirishwe kwa neema ya Ufufuko”.1 Maisha yote ya imani yetu yanatuelekeza katika tumaini la ufufuko. Katika kipindicha Kwaresima, imani inaimarishwa, matumaini ya kweli yanafufuliwa, upendo ulioanza kuchakaa unasafishwa na Pasaka ya milele inaandaliwa. Hiki ni kipindi ambacho Kanisa,kupitia Neno la Mungu na mazoezi ya kiroho, linatukumbusha na kutuelekeza kurudi na kulielekea lengo la juu kabisa la maisha yetu katika uhusiano mkamilifu na Mungu. Ukamilifu wa uhusiano na Mungu, ambao kwao uhusiano wote wa binadamu unaratibiwa, unajengwa juu ya msingi wa wemana haki. Ndio maana, katika maadhimisho ya Kwaresima ya mwaka huu, sisi Maaskofu wenu, tunapenda kuungana nanabii Isaya tukiwahimiza na kusema: “Zingatieni haki na kutenda mema” (Isa 56:1).

Kama jamii ya waamini, tumesimama mbele ya wajibu wa maisha ambao unadai ukomavu na ujasiri wa kiimani. Wajibu huu ni wa kutenda haki kwa nafsi zetu wenyewe, yaani;kuutafuta wokovu wetu, na kuwa wema kwa kuwatendea jirani zetu wote haki kila tunaposaidiana na kuelekezana katika mambo yote yampendezayo Mungu na kuijenga jamii.


Tafakari hii ya Kwaresima tunaileta kwenu ili pamoja tuzipime njia na mienendo yetu ili kuona ni kwa kiasi gani tunazingatia haki na kutenda mema mbele ya Mungu na mbele ya jamii. Ni kwa njia hiyo tu ndipo tunapoweza kutambua ni kwa kiasi gani tumefanikiwa “kuidhihirisha harufu ya kumjua yeye kila mahali kwa kazi yetu!” (2Kor 2:14). Kama bado hatujaanzakuzingatia misingi ya haki na wema, hii ni fursa ya kuanza mara moja. Na Mungu atatuimarisha na kutuokoa kwani yeyemwenyewe anatamka: “Ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jinalangu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, nakuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia kutoka mbinguni, nakuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao” (2Nya 7:14).

SURA YA KWANZA

HAKI

1 Zingatieni haki na kutenda mema ninyi ambao mlioitwa na Mungu na kukombolewa na Bwana Wetu Yesu Kristo mpate kufanywa wenye haki na kustahili kupokea memayote ambayo Mungu amewaandalia watu wake. Ujumbehuu ulikuwa ni onyo kwa viongozi wa Waisraeli wa kizazi kilichofuatia kile kilichotoka utumwani Babeli, kizazi kilichokuwa na matumaini makubwa ya kuishi maisha huru na ya mafanikio ambayo kwa bahati mbaya hawakuyapata kutokana na umaskini uliokithiri, manyanyaso na kusetwa mikononi mwa wachache. Maneno haya ambayo Mwenyezi Mungu anayatamka kupitia kinywa cha nabii Isaya ndio mwaliko ambao sisi Maaskofu wenu tunautoa kwenu Wanafamilia ya Mungu ili kila mwamini ajichunguze na kupima mwenendowake katika kuzingatia haki na kutenda mema. Msingi wa maisha yetu ni kumuonea Mungu kiu na kuishi katika njaa isiyokoma ya kutenda mema kwa ajili ya Mungu.

2 Mungu ni haki. Na kila inapotokea mwanadamu akatenda mema anakuwa ametenda haki. Haki ni “utashi wa kudumu wa kumpa Mungu na jirani iliyo haki yao”.2 Mungu na jirani ni sehemu ya lazima katika safari ya maisha yetu. Kuumbwa kwetu kwa sura na mfano waMungu (Mwa 1:26) kumetuweka chini ya wajibu wa kuwakielelezo cha haki na wema wa Mungu katika maisha yetu. Tunapoutimiza wajibu huu adhimu Mungu anaishibisha njaa yetu na kuponya kiu yetu (Mt 5:6). Kwa upendomkubwa Mungu aliiumba dunia na vyote vilivyomo nakwa haki yake anatawala dunia na kuiongoza.

Ni kwa wema na upendo mkubwa alimwumba mwanadamu na kumpa hadhi na heshima kubwa kati ya viumbe vyake vyote. Hata pale mwanadamu alipomkosea muumbawake, Mungu alimwadhibu kwa haki na kwa wema wake akaanzisha mpango mkubwa wa ukombozi. Mwenyezi Mungu aliendelea kuonesha upendo, wema na haki yake kwa taifa teule kipindi chote cha mahangaiko utumwani Misri na baadaye jangwani alipowaongoza wana waIsraeli kwa miaka 40.

Ni kwa wema, upendo na haki yake aliwainua waamuzi na baadaye manabii wapate kuwaelekeza watu wakena kwa mkono wa watawala aliwateua, aliwaongoza nakuwafanya taifa kubwa ingawa mara nyingi walimwachana kumwasi. Utimilifu wa upendo na wema wa Mungukwa wanadamu unaonekana katika nafsi ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyesulubiwa ili wanadamu wapate kuhesabiwa haki: “Kwa maana jinsi hii Mungualiupenda Ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee bali awe na uzima wa milele!” (Yn 3:16).

3. Kumjua Mungu ni kutenda haki (Yer 22:16). Ni katika huruma kuu na wema wake Mungu, Neno alifanyika mwili na kukaa kwetu nasi tukauona utukufu wake, amejaa neema na kweli. Katika maisha na utume wake Bwana Wetu Yesu Kristo alipita huko na huko akitangaza habari njema kwa maneno na matendo yake. Kwa hotuba ya mlimani anatoa ufupisho wa mafundisho yake; “heri walio maskini wa roho, maana ufalme wa mbinguni ni wao” (Mt 5:3-11) na kwa maneno ya nabii Isaya anadhihirisha na kutoa dira ya utume wake; “roho ya Bwana i juu yangu, kwa sababu Bwana amenitia mafuta,niwahubiri wanyenyekevu Habari Njema. Amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao” (Is 61:1). Kwa wema mkubwa anaponya wagonjwa, anafufua wafu, analisha wenye njaa na kwa huruma kuu anasamehe wenye dhambi. Ni katika mwanga wa haki ya kimungu Kristo anatetea wanyonge na kuwashutumumafarisayo na walimu wa sheria.

4. Kanisa lililo chombo cha wokovu wa wanadamu linabidishwa kupokea mwaliko wa kuzingatia haki nakutenda mema kama msingi wa utume wake kwa karne zote. Kanisa linao wajibu wa msingi kabisa wa kulindana kutetea haki na kujibidisha kwa huruma na ukarimu kuwatetea watu wote hasa wanyonge na waliosahaulika. Pamoja na jukumu hili, Kanisa linatambua kuwa linapaswa kuongozwa na kutekeleza utume wake kwa haki, upendo na ukarimu kwa wote. Ni katika mwanga huu jamii ya waamini katika ujumla wake na hatamwamini mmoja mmoja anaalikwa kuzingatia haki na kutenda mema kwanza kabla ya kutafuta haki na kudai kutendewa mema kama anavyofundisha Mt. Fransiskowa Asizi katika sala yake: “Ee Bwana unifanye chombo cha amani yako, nieneze mapendo palipo na chuki, walipokoseana nilete msamaha, nilete mwanga palipo na giza, nilete furaha palipo na huzuni… Ee Bwana unijalienitamani zaidi kufariji kuliko kufarijiwa, kufahamukuliko kufahamiwa, kupenda kuliko kupendwa”.

SURA YA PILI
UKUU WA HAKI NA TUNU ZAKE

1 Haki ni fadhila-tunu imwelekezayo mwanadamu na jamii kumtendea Mungu muumba wa vitu vyoteitakiwavyo kwa Umungu wake na wanadamu wenyewekutendeana ilivyo halali kwa hali zao. Katika haki zakijamii kunatakiwa pawepo taratibu na kanuni za kujenga mahusiano mema ya kumstawisha kila mtu ndani ya jamii. Lakini, mara nyingi haki inahatarishwa kwa mwelekeo wa kuweka mbele ubinafsi au upendeleo kwamakundi kwa malengo ya kujinufaisha na kuwatengambali wengine na mafao yaliyo halali yao. Haki ni zaidi yamikataba au misururu ya sheria na kanuni walizojiwekea wanadamu kukidhi vionjo vyao. Haki sharti itokane na utu wa mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Haki ikiwemo na ikizingatiwa kwa dhatikatika jamii wanajamii huendesha mambo yao kwa mshikamano, upendo na amani, maana bila haki hakuna amani.

2 Upendo ni tunu ya kwanza ya haki. Palipo na upendolazima haki itawale na palipo na haki pia upendo upo.Upendo ni wema unaovuka mipaka ya haki kwa ajili ya usitawi na furaha ya wote. Ni tunu itupayo kipimocha kuthaminisha maadili mengine yote katika jamii. Wanajamii wapendanao huwa huru na wa kweli wakitendeana kwa haki. Upendo hudhihirishwa kwamatendo mema.

Uhuru ni tunda jingine la haki. Uhuru ni ishara ya heshima kuu ya utu wa kila binadamu aliye sura na mfano wa Mugu akiwa na akili na utashi wa kulinda himaya aliyodhaminiwa na Mungu. Binadamu kuwa huru hakumaanishi kujitenga na asili yake bali ni kuishi katikamfungamano wa kujaliana kwa kila hali akiongozwa na ukweli na haki. Kilele cha uhuru wa mtu ni uwezo wake wa kujiamulia kutenda mema yatukuzayo utu wake na kumpa Mungu tukufu au kutenda maovu yadhalilishayo utu wake na kuiumiza jamii.

Matendo Mema kama ushuhuda wa imani.

7. Nyakati zetu, pengine kuliko nyakati nyingine zote za maisha na utume wake, Kanisa linashuhudia hitaji kubwa la maisha ya ushuhuda wa kiimani katika kutafuta haki na kutenda mema. Injili ya Kristo imehubiriwa nakupokelewa na watu wengi katika maeneo mengi, lakini hatuoni uwiano wa ongezeko la wanaomwamini Kristo na ongezeko la matendo mema, matendo ya huruma na kukua kwa upatikanaji na utoaji wa haki. Ni dhahiri kuwakumwamini Kristo ni kushika amri na maagizo yake; na agizo kuu analotupatia ni kupendana na kutendeana wema. Bwana anatuonya na kutufundisha kwa manenona mifano mbalimbali kama mfano wa tajiri na maskiniLazaro (Lk 16:19-31) na kama ilivyo pia kwa mfano wa hukumu ya mwisho -nalikua na njaa, ukanilisha, nalikuwa uchi ukanivika, nalikuwa na kiu ukaninywesha,nalikuwa mgonjwa ukaja kunitazama, nalikuwa mgeniukanikaribisha, nalikuwa kifungoni ukanijia (Mt 25:31¬46). Yakobo Mtume anasisitiza na kutuasa kwa maneno mazito: “Ndugu zangu kuna faida gani mtu kusema ana imani, lakini haoneshi kwa vitendo? Tuseme kaka au dada hana nguo na chakula, yafaa kitu gani kuwaambia hao: ‘Nendeni salama mkaote moto na kushiba,’ bila kuwapa mahitaji yao ya maisha? Vivyo hivyo imani bila matendo imekufa” (Yak 2:14-17). Tunawasihi na kuwaalika wanafamilia ya Mungu, kujali na kuwasaidia wahitaji na kuzingatia haki katika nyanja zote kuanzia katika familiazetu zilizo Kanisa dogo.

8. Pamoja na ukweli kwamba leo hii tunashuhudia ongezekola watu, makundi ya watu na taasisi zinazojishughulishana kuwasaidia wahitaji, lakini pia tunashuhudia wengiwa watu hao na taasisi hizo zikiwatumia wahitajiili kujinufaisha wao zaidi ya walengwa. Upendo kwa masikini haupatani na ubinafsi unaopelekeakujilimbikizia mali au matumizi yake ya choyo: “Haya basi, enyi matajiri! Lieni, mkapige yowe kwa sababuya mashaka yenu yanayowajia. Mali zenu zimeoza, namavazi yenu yameliwa na nondo. Dhahabu yenu na mali yenu zimeingia kutu, na kutu yake imewashuhudia, nayo itaila miili yenu kama moto” (Yak 5:1-3).

9. Ubinafsi na uchoyo uliokithiri unaathiri sana jamii yetu ya kitanzania kiasi cha kubadili hata mifumo ya kiutendaji ili kuwalinda wachache wenye mali na nguvu ya madaraka. Mwelekeo huu umeshusha thamani ya utuna kupumbaza fikra za wengi kiasi cha kuelekea kuamini kuwa bila mali na madaraka thamani ya mtu hushuka nakudidimia. Dhana hii imezaa hatari kubwa kwani utajiri, mali na madaraka vyaelekea kumeza malengo makuu yamaisha ya mwanadamu wa leo.

10. Kwa kujibidisha kutenda kazi za huruma, mwamini anakuwa ameonesha kwa matendo kile anachokiishi na kukiamini na kutoa ushuhuda wa imani yake. Kwa kazi na matendo ya huruma tunamsaidia jirani katika shida zake kiroho na kimwili. Matendo hayo ni pamoja na kufundisha, kushauri, kutuliza, kufariji, kusamehe nakusikiliza kwa utulivu (matendo ya huruma ya kiroho ). Pamoja na hayo, yapo pia matendo ya huruma ya kimwili ambayo ni pamoja na kuwalisha wenye njaa, kuwasitiriwasio na nyumba, kuwavika walio uchi, kuwatembeleawagonjwa na wafungwa na kuwazika wafu. Roho yenye kuzingatia haki na kutenda matendo mema ni kama taa iliyojaa mafuta ambayo hung’aa na kuangaza tayari kumlaki Bwana siku ya mwisho, bali roho isiyopambwa na matendo mema ni kama taa isiyo na mafuta ambayoimefifia na haiangazi (Mt 25:1-13).

11. Tunapoalikwa kuzingatia haki na kutenda mema, wakati huohuo, tunaalikwa kutafuta upatanisho kati yetu naMuumba na kati yetu sisi wenyewe kwa kuwa tayarikusamehe na kuomba msamaha pale tulipokosea. Nidhahiri kuwa Mungu ndiye asili na chimbuko la msamaha na kwamba ni vigumu kwa hulka yake, binadamu kuwezakusamehe kirahisi. Familia nyingi zinasambaratika kutokana na wanandoa kushindwa kutoa au kupokea msamaha. Kusamehe ni kutenda wema na kuzingatiahaki. Tusipokuwa tayari kuwasamehe walio tukosea, tunajifungia milango ya kupokea msamaha wa dhambizetu kutoka kwa Mungu mwenyezi. Mioyo yetu imekuwa migumu ikijitwika chuki, kinyongo na roho ya kisasi kwa waliotukosea japo kuwa hata sisi wenyewe si wenye haki mbele ya Mungu.

SURA YA TATU
MATUKIO YA KIKANISA

Sinodi ya Familia

12. Tukiwa bado tunakumbukumbu hai ya Sinodi ya Familia iliyofanyika mwishoni mwa mwaka jana huko Roma,tunapata nafasi ya kuendelea kutafakari na kujifunza juu ya chimbuko, asili na malengo ya familia kadiri ya mpango wa Mungu. Tunatambua kuwa familia hupata utambulisho na dhima yake katika mpango wa Mungu wauumbaji na ukombozi ikielekezwa juu ya kile inachowezakufanya na inachopaswa kutenda.3 Kila familia inapaswakutambua ndani mwake wito wake ambao hauwezi kupuuzwa, na ambao ni heshima na haki yake na wajibu wake mkuu. Tunapaswa kukumbuka daima kuwa, “mustakabali wa Kanisa na ubinadamu unazaliwa na kukua katika familia”.4 Kwa uelewa huo tunazialika familia kurudi daima kwenye lengo la mwanzo na la asili ya familia kama lilivyoratibiwa na Mungu. Hii ni fursa yakujifahamu na ya kuufahamu wito na utume wa familiaambao unapaswa kuwa dira ya kuongoza safari ya familia za kikristo zilizo msingi wa Kanisa lililo Familia hasa yaMungu.

13. Katika mpango wa Mungu familia ni jumuiya mwandani ya uhai na upendo ikiwa na dhima ya kudumisha uhai na upendo hadi kuufikia ukamilifu wake kama wote walioumbwa na kukombolewa wanavyotakiwakujitahidi. Familia ndiyo “hekalu la uhai wa binadamu” na chembe hai ya jamii, Kanisa na nchi yetu. Katika familia, baba, mama na watoto hujifunza mambo yote ya msingi kama kuheshimiana, kupendana, kusaidiana nakuwajibikiana.

Humo wote hubaini pia sura ya Mungu na iwapo mafunzo yote hayo yanakosekana, jamii nzimahuteseka kwa ukatili huo na huwa chimbuko la ziada yaukatili. Kila mfumo wa jamii unawajibu wa kuhakikisha familia zinawezeshwa kuendelea kuwa muhimili wa maisha bora na endelevu kiuchumi na kimaadili. Hata hivyo, jamii inawajibu wa kutambua kuwa familia ina haki zake ambazo hakuna anayeweza kuinyang’anya kwani zimetoka kwa Mungu mwenyewe. Ni katikafamilia mtoto anaweza kupata haki zake zote za mwilina roho na uhai wake kulindwa. Familia kama taasisi ya msingi kabisa inapaswa kulindwa ikianzia kulinda uhai wa wanafamilia toka kutungwa mimba mpaka kifo cha kawaida. Pasipo familia taifa halitakuwepo! Hata hivyo, familia zinapita katika kipindi kigumusana. Katika familia, ndiko tunakokuta manyanyaso na dhuluma kubwa wanazofanyiana wanafamilia pasipo udhibiti wowote.

Utamaduni wa uonevu haswakwa watoto na wanawake unajenga tabia za ukatili nauhalifu sugu katika familia kama taasisi asilia. Katika mazingira haya ni lazima tusimame na kuitetea taasisi ya familia kama ilivyoratibiwa katika mpango wa Mungu.Familia hujenga jumuiya ya watu, huhudumia uhai wawanajumuia na kupokea uhai mpya; ni mshirika mkuu wa kwanza wa maendeleo na ustawi wa jamii na mhusika mkuu katika dhima za Serikali na Kanisa. Kwa hiyo ni wajibu wa kila mmoja kuilinda familia. Mwaka huu pia, Kanisa litaendelea kutafakari nafasi na dhima ya familia katika Sinodi ya Kawaida ya Maaskofu itakayofanyikaRoma mwezi Oktoba 2015. Huu ni mwaliko wa kuzidi kujizamisha katika tafakari na mikakati ya kujenga na kulinda familia zetu ili nazo ziilinde na kuijenga jamii.

Mwaka wa Watawa

14. Baba Mtakatifu Fransisko ameutangaza mwaka huu Novemba 2014 – Februari 2016 kuwa Mwaka wa Watawa. Sisi Kanisa la Tanzania tumeupokea mwaliko huu kwa moyo wa shukrani tukitambua mchango mkubwa wa watawa katika utume wa Kanisa. Wapendwa watawa “twamshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu nyote… Wala hatuachi kuikumbuka kazi yenu ya imani, na taabu yenu ya upendo, na saburi yenu ya tumaini lililo katika Bwana wetu Yesu Kristo” (1 Thes 1: 1-5). Katika mwaka huu tungependa kuwahimiza watawa kurudi katika roho ya karama ya mashirika yenu. Litakuwa jambo la hatarikubwa kama shirika la kitawa litapoteza njia na kuiacharoho ya karama ya shirika. Mwaka huu uwe wa tafakari kwenu na kipindi cha kurudi daima kwenye chemchemi za maisha ya kikristo na za roho ya mwanzoni ya mashirika yenu.Tunapenda pia kuwahimiza mfanye bidii katika utume wenu ili mlipambe Kanisa, nalo limdhihirishe Kristo,“kwa waamini na wasioamini”,6 huku mkimpeleka na kumfikisha Kristo kwa watu.

15. Watawa kimsingi wanafanya kazi katika Kanisa mahalia. Uhusiano wa mashirika na uongozi wa majimbo naounapaswa uzidi kuboreshwa, ili huduma na utume wa Kanisa uzidi kuimarika.7 Utambuzi na umuhimu wa mashirika ya kitawa kutenda shughuli ndani ya jimboyakiwa yameunganika na uongozi wa Kanisa mahali ni wa kuzingatia sana.

16. Mwaka huu pia unapaswa kuwa fursa ya kutathiminina kuona ni kwa jinsi gani miito ya utawa inavyokua. Ni vema kuendelea kuhimiza miito. Namna ya kwanzaya kuhimiza miito iwe ni kwa mfano wa maisha yetu.Maisha ya kielelezo na ya kujitoa ni ya muhimu na hiindio namna bora ya kuufanya wito wa utawa uchanue nakupendwa. Vijana wakivutiwa kuingia utawa kwa sababu nyingine yoyote zaidi ya kumfanya Kristo apendwe naKanisa liendelee kutimiza wito wake, basi lengo lote la maisha ya utawa litapotea.

SURA YA NNE
WAJIBU WA KIJAMII WA KANISA

17. “Wito wa binadamu ni kudhihirisha sura ya Mungu”.8 Kanisa linazingatia wazo hili katika roho ya utume wake. Ni kwa sababu hii, Kanisa haliwezi kufumbia macho wajibu wake katika kuchangia makuzi ya jamii na kuhimiza “unyofu wa mwenendo”.9 Himizo la kuzingatia haki na kutenda mema, ni himizo linalolitaka Kanisa lijihusishe na jamii. “Mimi ni mwanadamu, hakuna suala linalomuhusu mwanadamu yeyote ambalo halinihusu”.10 Kila mara Kanisa linapotimiza wajibu huu linashutumiwa kuingilia siasa. Tafsiri hiyo ni potofu. Swali la kujiuliza ni hili kwamba, “siasa ni nini?”. Kama siasa ni mfumo wa maisha unaowahusu watu, Kanisa haliwezi kukaa pembeni. Kanisa likikaa pembeni litatenda dhambi ya kutotimiza wajibu kwa jamii. Kwani, “furaha na matumaini, uchungu na fadhaa ya wanadamu wa nyakati zetu, hasa ya maskini na wale wote wanaoteswa yote ni furaha na matumaini, uchungu na fadhaa ya wafuasiwa Kristo pia. Wala hakuna jambo lililo na hali halisi ya kibinadamu lisiloigusa mioyo yao”.11 Ni vema tuzidi kuwakumbusha wanakanisa kuwa wajibu wa kutetea nakulinda haki ni sehemu ya uinjilishaji na umisionari wa Kanisa. Hivyo basi, tusiruhusu kupokonywa furaha ya uinjilishaji na ari ya umisionari huu.

18. Dhana ya kudai kwamba Kanisa linaingilia siasa palelinapokosoa mifumo mibovu ya jamii ni upotoshajiwa makusudi. Hata hivyo, Kanisa Katoliki lingependa kutamka wazi kuwa wakati waamini wake wana vyama vyao vya siasa, Kanisa Katoliki halina wala halifungamanina chama chochote cha siasa. Kanisa linafungamana nabinadamu katika hali zake zote, njema na ngumu na lina wajibu wa kinabii wa kuwa “sauti ya wasiokuwa na sauti”. Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kuliasa Kanisa akisema: “Hutokea wakati mwingine kwambawahanga wa umasikini na kusetwa waamuapo kuanza kutenda kama watu wenye akili timamu na utashi na kudhubutu kukabiliana na vikwazo vya umasikini na manyanyaso, wawakilishi wa Kanisa hujiengua na kujifanya waangalizi tu. Kanisa sharti likubali kwamba maendeleo ya watu humaanisha maasi dhidi ya udhalimu. Iwapo Kanisa halitashiriki kwa vitendo katika maasi dhidi ya mifumo dhalimu ya kiuchumi inayosababisha watu kutoswa katika fedheha ya umaskini na kudhalilishwa, Kanisa halitakuwa na maana yoyote kwa watu na dini ya kikristo itapoteza mvuto na kuwa kamaushirikina ikikubaliwa kwa uoga tu. Iwapo Kanisa, waamini wake na asasi zake, halitadhihirisha upendo wa Mungu kwa watu kwa kushirikiana na watu na kwa kuwaongoza katika kupinga kiungwana maovu wanayotendewa na wadhalimu, basi litahusishwa na utesaji wa watu wote na kutokuwa na haki kwao. Jambo hili likitokea, Kanisa litakufa, na kwa kufikiri kibinadamu linastahili kufa”.13

19. Safari ya Taifa letu katika wakati wetu sasa ni safari inayopitia katika mkanganyiko mkubwa wa kutokujitambua na inayokosa utashi wa dhati wa kuijenga jamii inayokua katika misingi ya haki. Hii ni kwa sababu zipo dalili lukuki za kukosekana kwa uadilifu na dhamiri safi. “Hadhi ya binadamu yadokeza na kudai unyofu wa dhamiri adilifu. Dhamiri adilifu ni pamoja na kutambua misingi ya uadilifu”.14 Na kimsingi, “kadiri dhamiri inavyozidi kuwa nyofu, ndivyo watu na vikundivinavyozidi kujitenga na uamuzi kipofu na kujaribu (kuishi) kulingana na sheria halisi za uadilifu”.15

20. Kuinjilisha ni kuufanya uwepo wa Mungu ujidhihirishekatika ulimwengu wetu.16 Mungu, katika Kristo hamkomboi mtu mmoja mmoja tu, bali pia mahusiano ya kijamii baina ya watu.17 Ndio maana, katika moyo wa Injili tunaona uhusiano wa kina kati ya uinjilishaji na maendeleo ya mwanadamu.18 Tusiruhusu kupokonywa furaha ya uinjilishaji na umisionari huu.

Mchakato wa Katiba mpya

21. Taifa letu linapita katika kipindi cha mchakato wa Katiba mpya. Tunarudia kusisitiza kuwa hiki ni kipindi adhimu kwa Taifa letu. Tunapenda kulikumbusha Taifa letu kwamba hili ni zoezi linalodai uadilifu mkubwa na utashi wa kisiasa wenye lengo la kujenga Taifa kwa muda mrefu. Kejeli, vitisho, migomo, vijembe na kukosa ustahimilivu katika mijadala yenye kulenga kuunda misingi ya mustakabali mwema wa Taifa letu vinaonesha kukosekana kwa uzalendo na ukomavu wa kisiasa. Mchakato wa marekebisho ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania usiwe chimbuko na chanzo cha kubomoa mema mengi yaliyokwisha kufikiwa kwa amani, uhuru, udugu na haki. Ikumbukwe kwamba Katiba ni Mwongozo Mkuu na kiunganishi cha msingi chajamii yetu ya Tanzania.

Katiba mpya inapaswa kutujenga katika utamaduni na maisha mapya yatakayotokana na mila na desturi za makabila zaidi ya 130 kwa kujengamisingi mipya iliyosheheni dira mpya, miiko ya uongozi, haki, wajibu na uwajibikaji chini yake au kwa mujibu washeria, kanuni, mila, desturi na mapokeo ya jamii. Kwa nguvu ya katiba bora sisi sote Watanzania wa Bara na Visiwani tutaweza kuheshimiana kiadilifu, siyo kinafiki; na jumuiya ya kisiasa na wengine wote walio na mamlaka na nyadhifa za kiutawala na kiuongozi kuwajibikakidemokrasi.

Uchaguzi mkuu 2015

22. Mwaka huu wa 2015 ni mwaka wa Uchaguzi Mkuunchini Tanzania. Tutakuwa tunakabiliwa na uamuzi wa kisiasa kwa kuchagua viongozi watakaotumia rasilimaliza taifa letu kwa ama ustawi na maendeleo ya wengiwalio katika lindi la umaskini au kwa matumizi ya faharizao binafsi na wabia wao katika kujitajirisha. Tunashauri zoezi hili liendeshwe kwa uadilifu na lisifanywe kuwatendo la ulanguzi wa kura. Huku ni kudhalilisha utu wawatu na kuvuna madaraka kupitia umasikini wa watu.Tunapenda wale wanaoomba dhamana ya uongoziwa Taifa hili katika nyanja zote na sisi sote tunaotumia haki ya kura zetu tuitumie fursa hii kama dhamana na tendo la heshima ya utu wetu. Matukio haya ya makuzi ya jamii yetu yasidhoofishe amani yetu. Katika yote tunawahimiza; zingatieni haki na kutenda mema, mkitenda
yote kwa moyo huru unaoongozwa na dhamiri safi.

Hitimisho

23. Wapendwa Taifa la Mungu, sisi Maaskofu wenu tunawatakieni kila baraka katika safari hii ya imani.Tumwombe Mungu aithibitishe Imani yetu nayoijidhihirishe katika maisha na matendo yetu ya kila siku katika kuzingatia haki na kutenda mema.
Ni sisi Maaskofu wenu,
1. Mhashamu Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa Rais wa Balaza la Maaskofu Tanzania, Iringa
2. Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo - Dar es Salaam
3. Mhashamu Askofu Mkuu Josaphat Lebulu - Arusha
4. Mhashamu Askofu Mkuu Paul Ruzoka - Tabora
5. Mhashamu Askofu Mkuu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi OfmCap – Mwanza
6. Mhashamu Askofu Mkuu Damian Dallu - Songea
7. Mhashamu Askofu Mkuu Beatus Kinyaiya - Ofm Cap - Dodoma
8. Mhashamu Askofu Mkuu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi OfmCap – Ap. Adm Shinyanga
9. Mhashamu Askofu Telesphor Mkude - Morogoro
10. Mhashamu Askofu Gabriel Mmole - Mtwara
11. Mhashamu Askofu Bruno Ngonyani - Lindi
12. Mhashamu Askofu Anthony Banzi - Tanga
13. Mhashamu Askofu Agapiti Ndorobo - Mahenge
14. Mhashamu Askofu Evaristo Chengula, IMC - Mbeya
15. Mhashamu Askofu Augustino Shao, CSSp - Zanzibar
16. Mhashamu Askofu Damian Kyaruzi - Sumbawanga
17. Mhashamu Askofu Severine NiweMugizi - Rulenge-Ngara
18. Mhashamu Askofu Desiderius Rwoma - Bukoba
19. Mhashamu Askofu Desiderius Rwoma – Ap. Adm Singida
20. Mhashamu Askofu Method Kilaini, Askofu Msaidizi - Bukoba
21. Mhashamu Askofu Ludovick Minde, ALCP/OSS -Kahama
22. Mhashamu Askofu Alfred Leonard Maluma - Njombe
23. Mhashamu Askofu Castor Paul Msemwa - Tunduru-Masasi
24. Mhashamu Askofu Michael Msonganzila - Musoma
25. Mhashamu Askofu Issack Amani - Moshi
26. Mhashamu Askofu Almachius Rweyongeza - Kayanga
27. Mhashamu Askofu Rogath Kimaryo CSSp - Same
28. Mhashamu Askofu Salutaris Libena - Ifakara
29. Mhashamu Askofu Eusebius Nzigilwa, Askofu Msaidizi
-Dar es Salaam
30. Mhashamu Askofu Renatus Nkwande - Bunda
31. Mhashamu Askofu Gervas Nyaisonga - Mpanda
32. Mhashamu Askofu Bernadin Mfumbusa – Kondoa
33. Mhashamu Askofu John Ndimbo – Mbinga
34. Mhashamu Askofu Titus Mdoe, Askofu Msaidizi – Dar es Salaam
35. Mhashamu Askofu Renatus Nkwande – Ap. Adm Geita
36. Mhashamu Askofu Joseph Mlola ALCP/OSS - Kigoma
37. Mhashamu Askofu Prosper Lyimo, Askofu Msaidizi -Arusha.









All the contents on this site are copyrighted ©.