2015-02-07 07:57:53

Vitendo vya kinyama dhidi ya ubinadamu!


Tarehe 8 Februari, 2015 imewekwa kuwa siku ya sala na uhamasishaji kimataifa kuhusu swala la biashara haramu ya watumwa. Baraza la Kipapa la haki na amani kwa kushirikiana na umoja wa Wakuu wa mashirika ya kitawa ulimwenguni, wanawaalika Wanakanisa ulimwenguni kote kusali na kuhamasisha jamii juu ya tatizo sugu la utumiaji wa watu kama vyombo vya kujipatia mapato. RealAudioMP3

Tarehe 8 Februari kila mwaka ni sikukuu ya Mtakatifu Josephine Bakhita, huyu alikuwa mtumwa kutoka Darfur, Sudan ambaye alipowekwa huru akawa mtawa wa Masista wa Kanosa, na alitangazwa kuwa mtakatifu mwaka 2000 Papa Yohane Paulo II.

Lengo la siku hii ni kuhamasisha jamii na kusali ili haki za watu wanaotumiwa kama vyombo vya kujipatia mapato ziweze kutambuliwa na bihashara hii haramu iweze kukomeshwa. Papa Francisko katika Barua yake ya Kipapa Evangelii Gaudium anakumbusha kwamba bihashara ya binadamu inaathiri jamii zote ulimwenguni. “Ni kwa jinsi gani ningetamani watu wote tusikie sauti ya Mungu inayotuuliza: “Ndugu yako yuko wapi?” (Mw. 4:9).

Huyo ndugu yako anayefanywa mtumwa yuko wapi? Huyo kaka au dada yako anayeuzwa kwenye ukahaba yuko wapi? Huyo kaka au dada yako anayetumiwa na baadaye kuachwa afe kwenye maghala ya viwanda au kwenye mashamba, yuko wapi? Watoto wanaolazimishwa kuwa ombomba kwa ajili mapato ya watu wasio na dhamiri si tunawaona? Sasa kwanini tunajifanya hatuoni? Swala hili linatuhusu sisi wote.”

Watu wote, hasa wakatoliki popote waliko, katika majimbo yote ulimwenguni tukusanyike na kusali, tujitahidi kutoa mchago wetu ili watu hawa ambao hakuna anayetetea haki zao waweze kuona mwanga wa matumaini. Sisi wote hatuna budi kujitahidi kuchukua hatua madhubuti ili kukomesha kila sababisho la aina hii ya utumwa. Takwimu kuhusu tatizo hili zatuonyesha kuwa biashara hii inawahusisha watu takriban milioni 21, wengi wao wakiwa watu maskini wa kila rika na jinsia, wakimbizi, yatima wasio na ulinzi wowote.

Kadiri ya utafiti uliofanya na David Pegg mwaka jana (4 Juni, 2014) unaonyesha mambo ishirini na tano yanayosababisha kubaki mdomo wazi mbele ya hali hii ya biashara haramu ya watu:

Mwaka 2013, bei ya mtumwa mmoja ilikuwa wastani wa Dola za Marekani kati ya 90-100. Katika sehemu nyingi ulimwenguni 80% ya biashara ya binadamu ilihusisha ngono na 20% zilizobaki zilihusisha kutumikishwa katika kazi viwandani na mashambani. Mwaka 2013 idadi ya watumwa ulimwenguni ilikuwa kati ya milioni 20-30. Kati ya hao, takriban watu milioni moja walisafirishwa kuvuka mipaka toka nchi moja kwenda nyingine kimagendo. Asilimia 5. 70% ya hao walikuwa ni watumwa wa kike. 6. 50% ya hao walikuwa ni watoto.

Biashara ya watu ni ya tatu kwa ukubwa wa mapato ikifuatia mdawa ya kulevywa na biashara ya silaha. Biashara ya watu inazalisha takriban bilioni 33 kila mwaka na nusu ya mapato hayo hutoka kwenye nchi zilizoendelea kiviwanda. Hata katika biashara ya nguvu kazi, wanawake bado ni nusu ya idadi ya watu wanaouzwa utumwani.

Biashara ya viungo vya binadamu ni moja shughuli zinazoongezeka siku hadi siku hata kama hutajwa kwa nadra sana katika vyombo vya habari. Takriban watu 30,000 ya waathirika katika biashara ya ukahaba hupoteza maisha kila mwaka kwa ajili ya majeraha, magonjwa ya kuambukizwa na kwa kutelelezwa. Asilimia 80% ya watu wanaouzwa katika utumwa wa kingono wana umri wa chini ya miaka 24 na baadhi yao ni watoto ambao hawajafikia umrti wa miaka sita.

Mtuhumiwa katika biashara ya watu Ludwig “Tarzan” Fainberg aliyehukumiwa hivi katibuni anabaini kuwa: “Unaweza kumnunua mwanamke kwa Dola 10,000 za kimarekani na kurudisha mtaji wako ndani ya muda wa wiki moja; na baada ya hapo kila upatacho ni faida tu ikiwa mwanamke mwenyewe ni mrembo na bado kijana.” Kadiri ya utafiti uliofanywa nchini Uholanzi mwaka 2003, mtumwa wa ngono humletea mmiliki wake pato la kiasi cha Dola za kimarekani 250,000 kila mwaka. Mfanya biashara wa watumwa wa ngono aweza kupata faida mara ishirini kwa kila msichana aliyemnunua, ili mradi hakusababishiwa majeraha yanayoharibu urembo wake.

Kati ya matokeo ya kumalizika kwa vita baridi kati ya magharibi na mashariki ni kuongezeka kwa makundi ya waasi katika sehemu mbalimbali za dunia na makundi hayo kutumia watoto katika mapambano kati yao. Kadiri ya utafiti uliofanywa na mwandishi wa habari wa gazeti la Times uliofanyika mwaka 2009, kundi la Taliban limekuwa likiwatumia watoto wadogo walio na umri wa chini ya miaka saba katika mashambulio ya kujitolea mhanga.

Bei ya mtoto wa kujilipua inafikia kati ya Dola za kimarekani 7,000-14,000. Shirika la UNICEF linakadiria kwamba kiasi cha watoto 300,000 walio chini ya umri wa miaka kumi na nane wanatumika katika mapigano katika sehemu mbalimbali za dunia. Watoto wadogo wanauzwa katika soko la kimagendo na mapato ya biashara hiyo hugawiwa kati ya wafanya biashara, madaktari, wanasheria, maafisa wa uhamiaji na wengineo.

Watafiti mbalimbali wamebaini kuwa kadiri hali mbaya ya uchumi inavyozidisha makali yake ulimwenguni, bishara haramu ya watu inazidi kuongezeka. Biashara haramu ya watu ni kati ya shughuli za kijangili zinazoongezeka kwa kasi kuliko zote ulimwenguni. Makundi ya wafanya biashara haramu wanavutwa kufanya biashara ya watu kwa sababu mtu anaweza kuuzwa mara nyingi kuliko bidhaa nyingine yoyote.

Kuna idadi kubwa ya watumwa ulimwenguni leo hii kuliko wakati mwingine wowote wa historia ya binadamu. Mnamo mwaka 2013 wafanya biashara ya watu walipata kipato cha Dola za Marekani bilioni 32 na kuwapiku makampuni ya Nike, Google, Starbucks kwa pamoja.


Kama vile Masista Wakanosa walivyofaulu kumfanya Mtakatifu Josephine Bakhita aweze kubadili mtazamo na maana ya neno “Bwana”, kutoka katika hali ya kuwaelewa mabwana wa utumwa na kuona upendo usio mipaka wa Bwana wa mabwana; hata sisi katika siku hii ya sala hatuna budi kujitahidi kwa kila tuwezalo kubadili hali za mamilioni ya watu wanaoishi katika hali ya utumwa na kuwasaidia waweze kuona wanapendwa na kujali utu wao.

Katika ujumbe wake wa siku ya kuombea Amani Duniani mwaka huu 2015, Papa Fracisko amependa uwe na kichwa cha habari kifuatacho: “Toka sasa Utumwa uwe mwiko: sisi wote ni ndugu.” – “No longer Slaves but brothers and sisters”. Basi sisi wote tuunganishe nguvu na kuhakikisha kuwa hali hii ya utumwa inakoma na siku hadi siku jamii itambue kuwa ni mwiko kumfanya binadamu mwenzetu kuwa mtu na bidhaa ya kujipatia mapato.

“Ee Mungu, tunaposikia habari za watoto na watu wazima wakidanganywa na kupelekwa kwenye maeneo yasiyojulikana kwa madhumuni ya unyanyasaji wa kingono, wakilazimishwa kufanya kazi na viungo vyao vya mwili kutumiwa kama vyombo vya kujipatia mapato,mioyo yetu inajaa huzuni na roho zetu kuwa na hasira kwani utu wao na haki zao zapuuzwa kwa njia za ulag’ai, vitisho na nguvu. Twainua sauti zetu tukilaani tabia hii na biashara hii ya utumwa wa kisasa. Kwa maombezi ya Mt. Josefina Bakhita kizazi chetu kiweze kuona mwisho wa biashara hii haramu. Tupe hekima na ujasiri wa kusimama pamoja na wale ambao miili, mioyo na roho zao zimejeruhiwa, ili kwa pamoja tuweze kufanya kweli ahadi yako kwa kuwajaza hao ndugu zetu upendo utokao kwako. Hao maharamia wakashindwe na kurudi mikono mitupu wakatubu kutoka katika njia zao ovu. Tusaidie nasi tuweze kuwa vyombo vya uhuru ambao ni zawadi itokayo kwako kwa ajili ya wana wako. Amina.”

Na Padre Felix Mushobozi, C.PP.S.
Afisa kutoka Shirikisho la Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Italia.








All the contents on this site are copyrighted ©.