2015-02-06 08:36:24

Utume na Familia!


Wakurugenzi wakuu wa Mashirika ya Kipapa ya Kazi za Kimissionari kutoka Afrika ya Kati, kuanzia tarehe 9 hadi tarehe 15 Februari 2015 watafanya mkutano wao utakaoongozwa na kauli mbiu "Utume na familia: changamoto za kichungaji". Mkutano huu hufanyika kila baada ya miaka miwili, ili kuweka mbinu na mikakati ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya Mashirika ya Kipapa ya Kazi za Kimissionari.

Hii itakuwa ni fursa kwa wajumbe kuweza kubadilishana mawazo, changamoto na matarajio yao katika maisha na utume wa Kanisa mintarafu tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Tafakari hizi ni mwendelezo wa maadhimisho ya awamu ya kwanza ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia sanjari na maandalizi ya mwendelezo wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu familia, itakayofanyika mjini Vatican, mwezi Oktoba 2015, kwa kuongozwa na kauli mbiu "Wito na utume wa Familia ndani ya Kanisa na Ulimwengu mamboleo".

Padre Gaspard Mengata, Mkurugenzi mkuu wa Mashirika ya Kipapa ya Kazi za Kimissionari kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Cameroon anasema kwamba, kuna haja kwa Kanisa mahalia kupembua na kupyaisha mikakati na shughuli za kimissionari kwa Makanisa mahalia.

Ratiba inaonesha kwamba, wajumbe pamoja na mambo mengine, watajadili kuhusu utume kwa Mashirika ya Kitawa; Familia kadiri ya Mpango wa Mungu na uelewa wake mintarafu mila na desturi njema za Kiafrika; mchakato wa Uinjilishaji wa Familia, ili familia ziweze Kuinjilisha walimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha. Mkutano huu utahudhuriwa pia na Padre Ryszard Szmydki, Katibu mkuu wa Mashirika ya Uinjilishaji wa Watu.

Kuna Wamissionari wengi wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa Barani Afrika na kati yao, kuna wale wanaomimina maisha yao katika huduma. Itakumbukwa kwamba, kwa mwaka 2014 kuna Wamissionari na Watawa 7 waliopoteza maisha yao Barani Afrika: Watawa 3 wameuwawa kikatili nchini Burundi, kuna Mapadre wawili ambao wamepotea na hadi sasa hawajulikani mahali walipo huko Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati; Mtawa mmoja alitekwa nyara na hatimaye kuuwawa kikatili Afrika ya Kusini na mwishoni, kuna Mtawa mmoja aliyeuwawa kikatili katika tukio la ujambazi Dar Es Salaam, nchini Tanzania.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.