2015-02-05 08:26:20

Uchaguzi mkuu nchini Nigeria!


Kanisa Katoliki nchini Nigeria limejiandaa kikamilifu ili kushiriki katika mchakato wa uchaguzi mkuu, kwa kuwatuma waangalizi wa uchaguzi wapatao 4889 katika majimbo 23 ya uchaguzi, wakati wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini Nigeria hapo tarehe 14 Februari 2015. Wasimamizi kutoka Kanisa Katoliki wanaratibiwa na Padre Evaristus Bassey, Mkurugenzi wa Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki nchini Nigeria, Caritas sanjari na Tume ya haki, amani na maendeleo endelevu.

Viongozi wakuu wa dini nchini Nigeria wanahamasishwa kusaidia kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu wakati na baada ya uchaguzi mkuu nchini humo. Vijana wajiheshimu na kutunza amani na utulivu na kamwe wasikubali kutumiwa na baadhi ya wanasiasa uchwara ili kuchochea fujo na vurugu kwa masilahi yao binafsi. Wanasiasa wawe makini katika kampeni na kamwe wasiwe ni vyanzo vya fujo na machafuko wakati wa mchakato wa uchaguzi mkuu.

Wananchi wa Nigeria wanakumbushwa kwamba, ulinzi na usalama viko mikononi mwao, hata kama Serikali imeahidi kuhakikisha kwamba, kuna ulinzi na usalama wa kutosha wakati wa kupiga kura, lakini wananchi wenyewe wawe pia macho kwani vikosi vya ulinzi na usalama vinaweza kuzidiwa nguvu na matokeo yake yakawa ni majanga kwa watu na mali zao.

Viongozi wa kidini wanapaswa pia kujiandaa kwa kutenga fungu linaloweza kutumika kwa ajili ya kukabiliana na majanga, ikiwa kama yatatokea wakati wa uchaguzi mkuu, kwani hadi sasa hali ya usalama ni tete sana nchini Nigeria. Kwa miaka mitano sasa, kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram kimekuwa ni tishio kwa maisha na usalama wa wananchi wa Nigeria.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.