2015-02-05 11:05:01

Siku ya kuombea amani!


Maaskofu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaoshiriki katika mkutano maalum ulioandaliwa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yenye Makao yake makuu mjini Roma, unaoongozwa na kauli mbiu "Taifa la kinabii kwa ajili ya ubinadamu mpya", Alhamisi, tarehe 5 Februari 2015 kuanzia saa 12:30, kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria Trastevere mjini Roma, wataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuombea amani nchini Syria, Niger na Nigeria.

Baadhi ya Maaskofu wanatoka katika maeneo ambayo yameguswa na kutikiswa na vitendo vya kigaidi huko Syria ambako vita imepachikwa jina la kidini, ili kuendeleza nyanyaso na dhuluma dhidi ya watu wasiokuwa na hatia. Kuna Maaskofu kutoka Niger ambao hivi karibuni walishuhudia Makanisa yao yakichomwa moto kwa chuki za kidini, kama inavyojionesha hata Pakistan na Nigeria ambako Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram kinaendelea kupandikiza mbegu ya kifo, chuki na uhasama, madonda ambayo itachukua muda mrefu kabla ya kugangwa na kuponyeka kabisa!

Maaskofu wanasali ili kumlilia Mwenyezi Mungu awapatie amani na utulivu baada ya kipindi kirefu cha misiba na maombolezo. Maaskofu hawa wanasindikizwa na sala pamoja sadaka ya waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kwa kuwaomba wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa na wakuu wa nchi husika kuzivalia njuga changamoto hizi ili kuweza kupata suluhu ya kudumu. Wadau mbali mbali waguswe na mahangaiko ya watu wanaoendelea kuteseka kutokana na athari za vita pamoja na kulazimika kuyakimbia makazi yao.

Maaskofu hawa watakuwepo mjini Roma hadi tarehe 7 Februari 2015, wakati mkutano utakapofungwa na Maaskofu kuanza kurudi tena majimboni mwao, tayari kuendeleza mchakato wa ujenzi wa amani kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa wengi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.