2015-02-05 08:26:06

Msiwagawe wananchi!


Wananchi wa Riunione wanatarajiwa kufanya uchaguzi mkuu hapo tarehe 22 na tarehe 29 Machi 2015 ili kuwachagua viongozi watakaosaidia mchakato wa kukoleza maendeleo endelevu, kwani hii ni haki msingi ya kikatiba na sehemu ya utekelezaji wa demokrasia. Uchaguzi mkuu isiwe ni fursa ya kuwagawa watu, kuanzisha fujo na vurugu, kwani siasa inapaswa kujikita katika mchakato wa kutafuta na kudumisha mafao ya wengi.

Hii ni sehemu ya ujumbe ulioandikwa na Askofu Gilbert Aubry wa Jimbo Katoliki la Saint- Denis, kama sehemu ya maandalizi ya uchaguzi mkuu nchini humo na kwamba, kuna haja ya kuwachagua viongozi wanaonesha nia na ari ya kutaka kuwatumikia wananchi ili kuweza kukabiliana barabara na changamoto za maisha badala ya kuwachagua viongozi wanaotaka madaraka ili kujinufaisha wao wenyewe na ndugu zao.

Viongozi wa kisiasa waoneshe dira na mikakati ya kupambana na ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana wa kizazi kipya na kwamba, rasilimali na utajiri wa nchi usaidie kujenga na kuimarisha jamii; kwa kushirikiana na kusaidiana, kwani kimsingi siasa inapaswa kukoleza mafao ya wengi katika medani mbali mbali za maisha. Ni wajibu wa kila mwananchi kuhakikisha kwamba anashiriki kikamilifu katika ustawi na maendeleo ya nchi yake kadiri ya nafasi na dhamana yake ndani ya jamii. Kamwe nchi isigeuzwe kuwa ni msitu wa vita na machafuko; mahali ambapo binadamu kwa binadamu wanawindana ili kumalizana!

Askofu Gilbert Aubry anawataka waamini na wananchi kwa ujumla kuachana na falsafa ya kutaka kulipizana kisasi, kwa kujenga na kudumisha amani na maridhiano kwa kuanzia ndani ya mtu binafsi, familia na jamii katika ujumla wake. Mafao, utu na heshima ya binadamu vipewe kipaumbele cha kwanza katika dira na mikakati ya maendeleo ya wengi. Kanisa na Jamii vinapaswa kushirikiana ili kuhakikisha kwamba, kweli wananchi wanajipatia maendeleo ya kweli sanjari na kuendelea kutunza amani na utulivu!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.