2015-02-05 08:25:19

Furaha ya kweli inapatikana wapi?


Askofu mkuu Maurice Gardès wa Jimbo kuu la Auch, Ufaransa anasema, hata katika shida na mahangaiko, magonjwa na taabu, mwanadamu anaweza kuonja furaha na amani ya ndani, kinyume kabisa cha baadhi ya watu wanaodhani kwamba, mgonjwa hawezi kuwa na furaha eti kwa sababu ya ugonjwa wake. Hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya furaha ya mtu na udhaifu wake wa kimwili kutokana na ugonjwa.

Askofu mkuu Gardès anasema, ulimwengu mamboleo unakumbana na changamoto nyingi ambazo zinamwondolea mwanadamu ile furaha na amani ya ndani. Kati ya mambo haya kuna magonjwa: mateso, kuvunjika kwa ndoa, vita, ukosefu wa fursa za ajira pamoja na vizingiti vya maisha ya kawaida katika hija ya mwanadamu, kiasi cha kumwachia nafasi ndogo kabisa ya kuweza kufurahia ndoto na matamanio ya moyo wake.

Askofu mkuu Gardès anayasema haya yote katika barua yake ya kichungaji kwa Familia ya Mungu Jimbo kuu la Auch, Ufaransa, kama sehemu ya maandalizi ya Jumapili ya Wagonjwa, ambayo inafanyika jimboni humo tarehe 8 Februari 2015, ili kutoa nafasi kwa waamini kuweza kushiriki kwa wingi, ingawa, Siku ya Wagonjwa Duniani inaadhimishwa hapo tarehe 11 Februari 2015 sanjari na Kumbu kumbu ya Bikira Maria wa Lourdes.

Askofu mkuu Gardès anasema kuna haja kwa watu kutofautisha kati ya furaha na anasa, kwa kukubali na kuthamini hata udhaifu wa mwili wa mwanadamu. Inasikitisha kuona kwamba, kuna baadhi ya watu wanadhani kwamba, furaha ya kweli inajikita katika fedha na utajiri kwani waswahili wanasema, eti "fedha ni sabuni ya roho". Kuna watu wanadhani kwamba, furaha inapatikana katika ulimbwende, huko watu watajikwatua hadi kuchubuka, lakini wapi, bado utawakuta watu hawa hawana ile furaha ya kweli. Na wengine wanadhani kwamba, furaha inapatikana kwa njia ya mafanikio katika taaluma, hata huko nako, bado wanabaki wakiwa na midogo wazi! Wanashangaa na kupigwa na bumbuwazi! Maajabu ya Mungu.

Askofu mkuu Gardès anasema, unaweza kumkuta maskini hata katika umaskini wake anakicheko na furaha isiyokuwa na makunyanzi, kwani anaipokea na kuikubali hali yake ya ubinadamu na hivyo kuwa na amani na utulivu wa ndani mambo msingi katika maisha ya binadamu na wala si fedha, ulimbwende na mafanikio katika taaluma. Mwanadamu kwa kukubali mapungufu na udhaifu wake, anaweza kuishi kwa amani na utulivu, kwani mambo yote haya yanategemea jinsi ambavyo mtu mwenyewe anayakubali na kuyapokea katika safari ya maisha yake ya kila siku!

Askofu mkuu Gardès anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kufanya tafakari ya kina kuhusu Heri za Mlimani; muhtasari wa mafundisho makuu ya Yesu, ambayo ni kinyume kabisa cha utamaduni wa watu mamboleo wanaopenda anasa na starehe; watu wanaotaka "kula kuku kwa mrija, huku wakiwa wameketi kwenye viti virefu". Katika shida na mahangaiko ya ndani, mwanadamu anatafuta faraja na utulivu kwa wale wanaomzunguka; watu hawa wanakuwa ni dawa inayoganga madonda na hivyo kumkirimia mtu furaha na utulivu wa ndani.

Kuna haja ya kuendelea kufanya maboresho katika medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu, ili kweli dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi pamoja na kuhakikisha kwamba, watu wanawaonesha upendo na mshikamano wagonjwa na wale wote wanaoteseka kutoka na shida na magumu mbali mbali ya maisha. Wakristo wanahamasishwa na Mama Kanisa kuwasaidia na kuwahudumia wagonjwa, kwa kukubali udhaifu na mateso ya mwanadamu. Udhaifu wa mwanadamu na furaha ya kweli, vinapatikana kwa mwamini kuwa mfuasi mwaminifu na mkweli wa Yesu Kristo.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.