Baba Mtakatifu Francisco, akitoa mafundisho kwa mahujaji na wageni Jumatano hii mjini
Vatican, aliendelea na sehemu ya pili ya tafakari juu ya baba wa familia. Sehemu
ya kwanza, alizungumzia juu ya hatari za baba kuitelekeza familia, na leo alitazama
uzuri wa baba anayejali familia. Na alitazamisha maelezo yake kwa maisha ya familia
Takatifu ya Nazareti ya Yesu, Maria na Yosefu, akisema Mtakatifu Yosefu pia alipata
majaribu ya kutaka kumwacha Maria mchumba wake alipogundua kuwa yu mja mzito.
Lakini
malaika wa Bwana, aliingilia kati na kumfunulia kwamba ni mpango wa Mungu. Na Yosefu
kwa unyenyekevu, alikubali ujumbe huo na kuwa baba Mlishi wa Yesu. Yosef, mtu wa haki,
alisikiliza sauti ya Mungu kama ilivyoandikwa katika Injili ya Mt. 1:24" na kuendelea
na mpango wake na Maria akawa mkewe, na hivyo kuwa baba wa familia Takatifu ya Nazareti.Hili
linatoa fundisho jinsi baba anavyo takiwa kuisikiliza sauti ya Bwana katika maamuzi
yake, kutenda kwa hekima na haki daima.
Papa aliendelea kutoa tafakari juu
ya umuhimu wa baba akisema, kila familia inahitaji baba. Na alirejea pia baadhi ya
maandiko Matakatifu kutoka Kitabu cha Methali, maneno ya baba anayemrudi mwanae,
“Mwanangu, kama moyo wako una hekima, moyo wangu utafurahi hufurahi" Naam viuno
vyangu hufurahi, midomo yako inenapo mema( Mithali 23.15-16). Papa amesema aya hizo
hujumuisha wajibu wa baba ndani ya familia na jamii kwa ujumla kwa kizazi kipya.
Baba
mwema, daima huwafundisha watoto wake yaliyo mema kwa upendo na mshikamano wake yeye
mwenyewe. Ili hilo liwezekana Papa ameonya kwamba, ni lazima roho ya namna hiyo iumbike
kwanza kabisa, ndani ya moyo wake yeye mwenyewe, moyo wenye kuzingatia nidhamu na
taratibu adilifu za maisha na saburi, kama anavyotarajia pia watoto wake wawe.
Papa
alieleza na kuongeza kuwa, hakuna baba mwema asiye acha kuonea fahari, mtoto wake
anayekuwa na moyo wa hekima, mtoto anayemfanana katika kuzingatia mambo ya kweli katika
maisha. Baba ni kioo kwa mtoto wake, nao daima husema kwa watoto wao, ninaonea ya
kukuzaa, kwa kuwa umekuwa kama mimi. Na siku zote hufurahia kuona unatenda wa hekima
na haki. Hii maana yake ni juu ya uwezo wa kuhisi na kutenda lakini hata katika kuzungumza
na kutoa kuhukumu kwa hekima na uadilifu.
Baba Mtakatifu alieleza na kuitazama
jamii ya leo akisema katika nyakati hizi zetu ambamo uwepo wa baba ni kama haupo,
inakuwa ni jambo muhimu kwa baba kuwepo na kujishughulisha kikamilifu na maisha ya
kifamilia. Na jambo muhimu la kwanza kwa baba ndani ya familia ni kuwa karibu na mkewe
, kushirikiana na mkewe katika kila jambo iwe furaha au huzuni, matumaini na taabu.
Na wote wawili kwa pamoja, kuwa kufuatilia kwa ukaribu makuzi ya watoto wao.
Papa
alieleza na kusema ," Yesu anamtaja Mungu kuwa mfano wa Baba wote". Kama ilivyokuwa
kwa Mfano wa Mwana mpotevu, Mungu anasubiri kwa uvumilivu watoto wake waliopotea warejee
nyumbani , na kwa huruma na msamaha daima yuko tayari kuwapokea licha ya kumwasi.
Vivyo hivyo Baba Wakristo, wanapaswa kudumu katika kuyaiga maisha ya Mtakatifu Yosefu,
kutunza na kulinda familia zao, watoto wao na kuwafundisha yaliyo mema, kuirithisha
kwa uthabiti imani, na mema yote wanayoyasadiki.
Papa alikamilisha mafundisho
yake kwa kumwomba Bwana ili kwamba Kanisa, Mama yetu, katika nia zake zote, asaidie
kwa nguvu zake zote, kuonyesha maana uzuri na ukarimu wa baba kwa familia, kwa
sababu uwepo wao ni wa lazima kwa ajili ya makuzi ya vizazi vipya, wao baba wakiwa
watetezi na warithishaji wa imani, wema, haki na ulinzi kama alivyokuwa Mtakatifu
Yosefu.