2015-02-03 11:07:47

Ni hija ya amani!


Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, hija yake ya kichungaji mjini Sarayevo nchini Bosnia na Erzegovina, panapo majaliwa hapo tarehe 6 Juni 2015 inalenga kuwaimarisha Wakristo; kukuza na kukoleza mchakato wa kutafuta mafao ya wengi; kuimarisha udugu, amani, majadiliano ya kidini na urafiki kati ya watu. Hii ni hija ya tatu ambayo Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuifanya Barani Ulaya!

Akizungumzia kuhusu hija hii ya kichungaji ya Baba Mtakatifu huko Sarayevo, Askofu mkuu Luigi Pezzuto, Balozi wa Vatican nchini Bosnia na Erzegovina anasema kwamba, ni kutokana na kipaumbele cha pekee kinachotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; amana na hazina kuu kwa maisha na utume wa Kanisa. Habari ya ujio wa Baba Mtakatifu mjini Sarayevo imepokelewa kwa mikoni miwili na kwamba, ni hija ambayo itachangia kukoleza ustawi na maendeleo ya wananchi wa Bosnia na Erzegovina.

Mji wa Sarayevo uko njia panda na muhimu sana katika mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekumene, sanjari na majadiliano ya kitamaduni kwani hapa kuna mchanganyiko wa tamaduni za watu mbali mbali; ili kujenga na kukoleza mchakato wa haki, amani, upatanisho na umoja wa kitaifa. Baba Mtakatifu anapenda kukutana na Familia ya Mungu sehemu mbali mbali za dunia, ili kujenga na kukoleza utamaduni wa watu kukutana, ili waweze kuheshimiana na kuthaminiana, daima akitoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wale wote wanaoishi pembezoni mwa jamii.

Waamini wanaendelea kuhamasishwa ili kusali kwa ajili ya kuombea hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko huko Sarayevo, ili kweli iweze kuzaa matunda yanayokusudiwa katika medani mbali mbali za maisha ya wananchi wa Bosnia na Erzegovina, lakini zaidi amani na utulivu, upendo na mshikamano, vikolezo vikuu vya maendeleo.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.