Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Jumamosi jioni tarehe 31 Januari
2015 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Chuo cha Kipapa cha Wajerumani kwa
ajili ya kumshukuru Mungu kwa kumwezesha Kanali Daniel Anrig, mkuu wa Vikosi vya Ulinzi
na Usalama vya Kipapa kuhitimisha utume wake mjini Vatican na tayari kuanza awamu
nyingine ya maisha.
Itakumbukwa kwamba, Kanali Anrig alianza mkataba wake mjini
Vatican kunako tarehe 30 Novemba 2008. Vatican inamshukuru na kumpongeza kwa huduma
makini aliyoitoa wakati wote alipokuwa Kamanda mkuu wa Vikosi vya wanajeshi kutoka
Uswiss, al maarufu kama Swissguards. Ametekeleza dhamana hii kwa kuwajibika, katika
hali ya unyofu, uaminifu na ushirikiano mkuu na wadau mbalimbali katika vikosi vya
ulinzi na usalama mjini Vatican. Amekabiliana na matatizo, changamoto na fursa mbali
mbali, lakini akatoa majibu makini yaliyojikita katika imani na tunu msingi za maisha
ya kiroho na kiutu, daima akitegemea tunza na ulinzi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Katika
mahubiri yake, Kardinali Parolin amewataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema
kuendelea kujitaabisha kumfahamu Yesu Kristo, ili hatimaye, kujenga mahusiano ya kweli
na mema, ili kufahamu na hatimaye, kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yao.
Yesu aliosha madaraka katika kufundisha na kutenda kama sehemu ya utekelezaji wa utume
na wajibu wake. Hakukata tamaa alipokutana na magumu na hata kutakiwa kutoa maamuzi
machungu katika maisha. Alifahamu mahitaji ya wasikilizaji wake na kuwafunda kadiri
ya mapenzi ya Mungu.
Yesu Kristo, Masiha na Mkombozi, alikuja duniani ili kumkomboa
mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti, kwa njia ya Fumbo la Msalaba, akaonesha
ushindi dhidi ya shetani kwa kufufuka kutoka katika wafu, changamoto kwa waamini kujenga
na kudumisha mahusiano ya kweli na dhati na Kristo Yesu.
Kardinali Parolin
anawaalika waamini kujiuliza kuhusu mahusiano yao na Yesu Kristo, ikiwa kama kweli
wamemkubali kama Mwana wa Mungu aliyekuja kuwakomboa au wamebaki wakipigwa na bumbuwazi
kutokana na miujiza aliyokuwa anatenda, bila kumpatia nafasi ya kuingia katika maisha
na mioyo yao?
Liturujia ya Neno la Mungu, Jumapili ya Nne ya Kipindi cha Mwaka
B wa Kanisa inamwonesha Yesu anyefundisha na kutenda kwa mamlaka, kielelezo makini
kitakachopata utimilifu wake pale juu Msalabani. Kanisa linawashukuru kwa namna ya
pekee wanajeshi kutoka Uswiss ambao wamekuwa wakijisadaka kwa ajili ya ulinzi na usalama
wa Baba Mtakatifu mjini Vatican, utume wanaoutekeleza kwa imani na sadaka kubwa ya
maisha.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican.