2015-02-02 07:41:16

Nyanyaso dhidi ya wasichana na wanawake!


Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kujadili na kuibua mbinu mkakati inayoweza kutumika kwa ajili ya kung’oa ukatili unaofanywa dhidi ya wasichana na wanawake katika mapambano ya silaha sehemu mbali mbali za dunia; hali ambayo kwa sasa inazidi kushamiri kwa kasi ya ajabu.

Wasichana na wanawake ndio waathirika wakuu katika mapambano ya silaha, kutokana na mfumo dume ambao bado unaathari kubwa katika kulinda na kutetea haki msingi za wanawake na wasichana duniani. Unyama na ukatili huu unajionesha kwa namna ya pekee katika nyanyaso za kijinsia, utumwa wa ngono sanjari na biashara haramu ya binadamu, mambo ambayo ni kinyume cha utu na heshima ya binadamu kadiri ya Mafundisho Jamii ya Kanisa.

Kanisa linaamini na kufundisha kwamba, binadamu wote ni sawa kwani wameumbwa kwa sura na mfano wa Mwenyezi Mungu, wana utu na heshima inayopaswa kulindwa na kudumishwa, kumbe, nyanyaso dhidi ya binadamu ni kinyume kabisa cha utu na heshima yake. Huu ni mchango uliotolewa na Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa na kusomwa kwa niaba yake na Monsinyo Janusz Urbanczyk kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, katika kikao chake kilichohitimishwa hivi karibuni mjini New York, Marekani. Nyanyaso za kijinsia ni mambo ambayo yanaacha madhara ya kudumu kwa waathirika.

Ujumbe wa Vatican unakazia kwamba, vita ni kati ya mambo ambayo yanaathari kubwa katika mchakato wa ulinzi na usalama wa jamii husika na kwamba, familia zinaathirika vibaya zaidi, kwani mara nyingi watu wanalazimika kuyakimbia makazi yao, hali inayopelekea familia kusambaratika na hatimaye, kunyonywa zinapokuwa ugenini. Bila ulinzi wa kutosha, haki msingi za binadamu zitaendelea kuwekwa rehani chini ya mtandao wa vitendo vya kigaidi.

Inasikitisha kuona kwamba, Jumuiya ya Kimataifa inashindwa kutoa ulinzi wa kutosha kwa wanawake na wasichana kutokana na imani yao, hali ambayo inatishia amani na usalama wa Wakristo katika baadhi ya maeneo duniani. Hapa kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa, Serikali husika na viongozi wa kidini kulaani vikali mashambulizi yanayofanywa kwa misingi ya kidini.

Baba Mtakatifu Francisko, anaendelea kusema kwamba, biashara haramu ya binadamu inazidi kukua na kushamiri, jambo ambalo ni uhalifu dhidi ya ubinadamu. Hapa kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kujifunga kibwebwe ili kuhakikisha kwamba, biashara haramu ya binadamu inakomeshwa, kwani inagusa utu na heshima ya binadamu.

Kanisa Katoliki kwa njia ya Mashirika na Taasisi zake, litaendelea kutoa msaada wa hali na mali kwa waathirika wa biashara haramu ya binadamu pamoja na kushirikiana na Jumuiya ya Kimataifa, ili kukomesha biashara hii. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kukata katu katu utamaduni wa utumwa mamboleo, kwa kujielekeza zaidi katika ujenzi wa amani kwa kujikita katika Injili ya Uhai sanjari na kuhakikisha kwamba, Jumuiya ya Kimataifa na Serikali husika zinatekeleza dhamana na wajibu wake barabara.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.